Thursday, January 17, 2013

Yesu Mwenyewe Asema na Mwanamke wa Kiislamu



Mungu alinijibu Mimi!

Huu ni ushuhuda wa kweli kuhusiana na maisha ya mtu aliyekuwa anamtafuta Mungu.

Habari yako na Mungu akubariki. Jina langu ni Amal na ninashuhudia kwamba kile ambacho unaenda kusoma ni cha kweli kabisa na sahihi kwa kadiri ya kumbukumbu zangu maana Mungu mwenyewe ni shahidi yangu. Maombi yangu ni kwamba Mungu aseme  na moyo wako na kutumia ushuhuda huu kukubariki wewe kwa namna ya pekee maishani mwako.

Kimsingi mimi nilikulia kwenye familia ya Uislamu mkali. Baba yangu ni Mpalestina kutoka Israeli. Mama yangu ana asili ya Brazili. Alikuwa ni Mkatoliki. Baba yangu alikutana naye Brazili. Walioana na mama yangu alibadili dini na kuwa Mwislamu.

Kama ilivyo kwa watu wengi wanaohamia Marekani, familia yangu nao walikuja hapa ili kutafuta maisha bora. Walikaa Los Angeles ambako ndiko nilikozaliwa mwaka mmoja baadaye.  

Niliamini kila kitu nilichofundishwa kuhusu Uislamu na niliamini kuwa dini yetu ilikuwa bora kuliko dini zingine duniani. Ingawaje, kadiri nilivyokua, baadhi ya mafundisho ya Uislamu yalianza kunikera, kwa mfano kuvaa mavazi yanayokufunika kabisa. Sikuelewa kwa nini nivae nguo zenye mikono mirefu, yaani ni kwa vipi mwanamume atatamanishwa na kiwiko change, kwa mfano? Kisha kulikuwa na taratibu za swala. Sikupenda kusema kitu kilekile tena na tena. Nilijisikia kama mambo ya ajabu na kutengwa mbali na Mungu. Nilifundishwa kwamba ukimwomba Mungu kwa Kiarabu, basi utasikiwa zaidi. Lakini sikuwa na uwezo wa kuzungumza lugha hiyo, hivyo nilijisikia kama nimeachwa nyuma. Nilijaribu kuziandika sala za Kiarabu kwa Kiingereza, lakini bado kulikuwa na kitu kimepunguka. Nilitamani kuomba kutokea moyoni mwangu, na si kutokana na maneno ambayo si yangu.

Mafundisho mengine nayo yalinikera kama vile kuzuiwa kula baadhi ya vyakula – lakini kubwa lililonikera zaidi ni suala la kuwa na wake wengi mbinguni. Nilimwuliza baba yangu kama nilikuwa naenda mbinguni lakini hakunijibu. Alibaki kimya tu kuhusu swali lile. Nikiwa tineja, niliwaza, “Sitaki kabisa kuwa mbinguni halafu niwe mmojawapo kati ya kundi la wanawake wa mwanamume fulani … wazo tu lenyewe lilifanya mwili wangu usisimuke. Hapana. Hakika kabisa nilijua kuwa sitaki kwenda kwenye “mbingu” ya aina hiyo.

Mwaka 1981, nikiwa na miaka kumi na nane, nilifanya uamuzi wa kuolewa na binamu yangu wa kwanza ili tu kuiridhisha familia yangu. Siku zote nilipenda kuwafurahisha familia yangu, hasa baba yangu. Sikuwahi kwenda kwenye muziki wa dansi nikiwa sekondari au kuwa na rafiki wa kiume, maana hayo yalikuwa kinyume kabisa na matakwa ya baba yangu. Lakini miezi miwili tu baada ya kumaliza sekondari, niliolewa. Hata hivyo,  katika hali inayokatisha tamaa, hata jambo hili halikuonekana kumfurahisha baba yangu.

Mwaka 1985 nilijiandikisha kwenda chuoni kinyume na mapenzi ya mume wangu na baba yangu. Wao waliona kuwa sehemu yangu inapaswa kuwa nyumbani na jikoni ‘ambako mwanamke anatakiwa kuwa.’ Kwa makubaliano kwamba nitafanya wajibu wangu wote wa ‘mke’ nyumbani, nilikubaliwa kuendelea na chuo.  Tayari nilikuwa na ujauzito wa mwanangu wa kwanza na wa pekee. Nilipata mtoto mzuri wa kiume. Huenda haya yalikuwa na mashindano makubwa kabisa maishani mwangu, lakini nilifanikiwa kumaliza kazi zangu za nyumbani na kushinda tuzo mbili shuleni, nikawa mama, na hatimaye nilihitimu chuo. Ninapotafakari sasa, najua kuwa niliyafanya hayo yote ili kumfurahisha baba yangu, lakini bado haya nayo hayakuonekana kumfurahisha.

Ilikuwa ni mwaka 1991 nilipokuwa kwenye safari ya kikazi pamoja na mume wangu. Alikuwa ameanzisha biashara ya kuuza nguo kwenye maonyesho kwenye majimbo. Mume wangu, mimi pamoja na rafiki yetu, ambaye nitamwita “John” ili kutunza usiri, tulisafiri kwenye majimbo mbalimbali. Tulilala kwenye mahoteli na kufanya kazi kwa saa 16-18 kwa siku.

Oklahoma kilikuwa ni kituo chetu kinachofuata. Tulikuwa na saa 14 mbele yetu za kusafiri kwa gari na ilibidi kuondoka harakaharaka ili kufika kule kwa wakati ili kuweka kila kitu sawa kwa ajili ya maonyesho yale. Nilitamani kuwa na kitu cha kusoma kwenye safari hii ndefu, lakini sikuwa na chochote na hatukuwa na muda wa kusimama kwenye duka. Ili kuepuka kukaa tu kwa muda wote ule, niliamua kuchukua Biblia ya kahawia iliyokuwa kwenye chumba cha hoteli tulikolala.  Nilipofika mlangoni ili kuondoka, rafiki yangu John alinisimamisha na kusema, "Amal, haujawahi kuiba kitu maishani mwako na sasa unataka kuanza wizi, tena kwa Biblia? Hautafanya hivyo. Uko sawa?”

Nilicheka.  “John, hii ni Biblia tu. Hakuna mtu atakayeona kwamba kuna kitu kimepungua. Hakuna mtu anayesoma vitu kama hivi. Na hata hivyo, naiazima tu. Nitairudisha kwa njia ya posta.”

Kisha John akasema, "Nilidhani wewe ni Mwislamu. Kwa nini unataka kusoma Biblia ghafla kiasi hiki?”

Nikasema, “Unajua, nina shauku tu ya kujua inasema nini na licha ya hivyo, hakuna kitu kingine cha kusoma tutakapokuwa kwenye hii safari.”

Baada ya kusema hayo, sote tukaingia kwenye gari na kuanza safari yetu ndefu. Tukiwa garini, kwa takribani saa nzima, nikawa najisikia kuchoka tu. Nilikaa kwenye kiti kidogo katikati ya John (aliyekuwa anaendesha) na mume wangu aliyekuwa amekaa kwenye kiti cha abiria. Nilikuwa natazama kwa ushangao miali ya jua lililokuwa linatua ilivyokuwa ikitoa rangi mbalimbali kwenye mawingu. Wakati huohuo nikaanza kuimba wimbo nilioukumbuka wa utotoni … "Utukufu, utukufu, haleluya, utukufu, utukufu, haleluya." Kisha nikaacha kuimba kwa kuwa sikuweza kukumbuka maneno mengine. Tulikuwa tunapita mahali pazuri sana ambapo nilimshukuru Mungu kwa kupaumba. Halafu nikaimba tena maneno yale huku nikiwa sijui yana maana gani lakini kwa namna fulani, nilijua kuwa yanamwinua Mungu kwa ajili ya uumbaji wake. 

Kutokana na kushindwa kukumbuka maneno yaliyobakia ya wimbo ule, nikaomba, “Mungu nifundishe wimbo mpya wa kukuimbia wewe.” Niliyatazama mawingu huku nikiwaza hakika atanijibu. Lakini ah, sikusikia sauti kama radi ikija kutokea mawinguni kama ambavyo nilikuwa nikiwaza hivyo ndivyo Mungu anavyoongea. Ghafla, niliwaza jinsi nilivyokuwa mpumbavu, maana nilifundishwa kwamba Mungu huwa hazungumzi na yeyote. Niliitazama ile Biblia niliyokuja nayo ambayo ilikuwa miguuni mwangu na nikaifungua. Nilikuwa nimeamua kuwa nitasoma ukurasa wowote nitakaofungua kwanza. Na hiki ndicho nilichosoma:

Zaburi 108
wimbo au Zaburi ya Daudi.
1  Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Nitaimba, nitaimba zaburi, Naam, kwa utukufu wangu.
2  Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri.
3  Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, Nitakuimbia zaburi kati ya mataifa.
4  Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni.
5  Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako.
6  Ili wapenzi wako waopolewe, Uokoe kwa mkono wako wa kuume, uniitikie.
7  Mungu amenena kwa utakatifu wake, Nami nitashangilia. Nitaigawanya Shekemu, Nitalipima bonde la Sukothi.
8  Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu, Na Efraimu ni nguvu ya kichwa changu. Yuda ni fimbo yangu ya kifalme,
9  Moabu ni bakuli langu la kunawia. Nitamtupia Edomu kiatu changu, Na kumpigia Filisti kelele za vita.
10  Ni nani atakayenipeleka hata mji wenye boma? Ni nani atakayeniongoza hata Edomu?
11  Ee Mungu, si Wewe uliyetutupa? Wala, Ee Mungu, hutoki na majeshi yetu?
12  Utuletee msaada juu ya mtesi, Maana wokovu wa binadamu haufai.
13  Kwa msaada wa Mungu tutatenda makuu, Maana Yeye atawakanyaga watesi wetu.

Ilikuwa ni ajabu sana, lakini nilihisi kuwa kwa namna fulani Mungu alikuwa akizungumza na mimi kupitia kile nilichosoma. Kutokana tu na udadisi, nilitazama ukurasa niliokuwa nikisoma. Nikakuta ni ukurasa wa 666. Ha! Nilifunga kitabu kile haraka sana, maana nilikumbuka mafundisho yote kuhusu shetani na namba yake 666.  "Hivi Mungu anataka kuniambia kuwa kitabu hiki ni cha kishetani?" niliwaza.

Baada ya kutafakari kwa muda, nilifikia uamuzi kwamba vitabu vyote vyenye kurasa nyingi ni lazima viwe na ukurasa wenye namba hiyo. Huku nikijiona kama mjinga, nilitupilia mbali wazo lile la kwamba Biblia ni kitabu cha kishetani.

Siku chache baadaye kule Oklahoma, niliugua mafua makali sana. Nikawa najisikia kizunguzungu na siwezi kutembea. Hivyo nilibakia kwenye chumba cha hoteli huku mume wangu na John wakiwa kwenye biashara. Nilikuwa peke yangu nimelala kitandani kwenye chumba hiki ambacho kilikuwa na mwanga hafifu. Nilianza kuwaza mengi na jinsi maisha yangu yalivyo magumu. Nilikuwa sina furaha. Nilitamani sana kumwona mwanangu maana nilikuwa sijamwona kwa mwezi mzima. Nami sasa nilikuwa hapa eti kwenye “safari ya kibiashara.” Mume wangu hakuwa mfanyabiashara mzuri sana. Kila wakati alikuwa ni mtu wa kutafuta mafanikio yasiyopatikana. Nilipiga hesabu na kukuta kwamba kila siku tulikuwa tunapoteza dola 400, lakini hata hivyo hatukuwa na uwezo wa kuondoka maana tulikuwa tumefungwa na mkataba wa maonyesho yale. 

Hili pamoja na matatizo mengine maishani mwangu yalianza kupiga kelele ndani ya kichwa changu. Niliamua kwamba, kama nikiendelea kuwaza juu ya matatizo yangu, itakuwa hatari kwa afya yangu. Baada ya hapo nilikamata rimoti na kuwasha TV. Nikawa natafuta chaneli ya sinema au nyingine ambayo ingenisahaulisha mawazo yangu. Hata hivyo nilikuwa nimeshachelewa. Nikaanza kulia na kwa hasira nilitupa ile rimoti kitandani na TV ikawa inabadili chaneli yenyewe.  Sikujua imeshia kwenye chaneli gani maana macho yangu yalijaa machozi.

Wakati naendelea kulia, nilimsikia mtu kwenye TV akisema jambo kuhusiana na Yesu. Mara moja niliwaza, “Aha, vizuri. Hicho ndicho ninachohitaji kwa sasa. Mmoja wa wale wahubiri wa kwenye TV walio na wazimu.” Kutokana na kujihurumia, nililia hata zaidi huku huyu mwanamume akiendelea kuzungumza. Alisema, “Unajisikia kuchanganyikiwa kwa sababu una matatizo mengi.”
Huku nikiendelea kulia, nilikubali na kusema,  "Ndiyo, ninajisikia kuchanganyikiwa na nina matatizo mengi sana."
Kisha akasema, "Unalia na umekata tamaa."
Nami nikajibu kwa sauti, "Ndiyo, ninalia na nimekata tamaa."


Ilikuwa ni hapo ndipo nilipoamua kuinua macho yangu ili nione ni nani huyo aliyekuwa akiongea nami. Kwa hiyo nilikaa kitandani na kuchukua tishu ili nifute machozi yangu niweze kumwona vizuri huyo mtu kwenye  TV. Ndipo alipaza sauti akisema, "Hivi sasa umeshakaa!"
Nilianza kulia hata zaidi na kwa sauti huku nikifunika uso wangu kwa mikono na kutikisa kichwa changu kulia na kushoto.
"Ndiyo, nimekaa," nilijibu.
Kisha akasema, "Umeweka mikono yako usoni kwa namna hii na unatikisa kichwa chako namna hii.”


Nilivuta pumzi ya ghafla na nikakodoa macho kwa nguvu sana kwenye TV wakati mwanamume yule akiwa anaiga vitendo nilivyokuwa navifanya. Sikuamini macho yangu. Alikuwa anaongea na mimi!
Kisha akasema kwa sauti ya juu huku amenyoosha kidole chake moja kwa moja kwangu kupitia TV, “Mwanamke, Yesu ndiye jibu lako! Njoo moja kwa moja kwenye TV yako!”

Bila kujiuliza lolote niliruka kutoka kitandani na kukimbilia kwenye TV ambapo nilipiga magoti mbele yake. Ukumbuke kwamba kabla ya hapa nilikuwa siwezi kutembea lakini sasa kwa namna fulani niliweza kuruka kwa ghafla kiasi kile.
Akasema, "Haraka, hakuna muda wa kupoteza. Weka mikono yako kwenye mikono yangu na urudie nitakachosema.” Aliinua mkono wake na kuelekeza kiganja chake kwangu. Nilipogusisha mkono wangu katika mkono wake kwenye TV, alisema, "Sasa rudia baada yangu."

Ndipo alianza kusema kile ambacho leo ninakijua kama “sala ya toba.” Kwa namna fulani nilijua kutokea ndani yangu kwamba hii ilikuwa ni njia ya kuelekea kwa Mungu.

Alianza kuongea harakaharaka huku mimi nikijaribu kuwa makini sana kwenye maneno aliyosema.

Unajua, kwenye Uislamu nilifundishwa kwamba kama nisiposema sala kwa usahihi, Mungu hataipokea. Nilipoanza kurudia baada yake, kile ninachoweza kusema ni kuwa, mwanga wa buluu ulipenya katikati kabisa ya kiganja changu kilichogusa skrini ya TV. Mwanga ule ulipita kwenye mkono wangu, ukapanda mabegani, na kichwani, na ukashuka miguuni lakini upande wa kulia tu wa mwili wangu. Kisha ukahamia upande wa kushoto. Ilikuwa ni kama nguvu fulani iliyo nzuri.

Halafu hii nguvu ya mwanga wa buluu ilianza kwenda kimzunguko ndani ya mwili wangu na kuanza kukua ikitoka nje. Kisha ikaanza kumwagikia kwenye chumba kile ambacho kilikuwa na nuru hafifu. Sikuwa na hofu hata kidogo na nilijua kuwa hili lilikuwa ni jambo zuri. Lile duara la mwanga lilikua na kuwa kubwa na rangi yake ikawa nyepesi hadi chumba chote kikajawa na nuru nyeupe. 

Hisia za upendo ambazo sikuwahi kukutana nazo zilinifunika. Nilijisikia niko salama. Kwa namna fulani, nilijiona nimekuwa kitu kimoja na ile nuru. Nikajua wazi kuwa huu ulikuwa ni wakati ambapo nimewahi kuwa karibu kabisa na Mungu kuliko wakati mwingine wowote.

Kila kitu kilipofikia mwisho, yule mwanamume wa kwenye TV alisema tupige simu kwa namba iliyokuwa kwenye skrini kama mtu umesema ile sala. Mara moja nilinyanyua simu na kupiga ile namba. Sauti tamu ya mwanamama iliitikia. Alinipongeza kwa kumpokea Yesu moyoni mwangu. Nami nikasema, “Asante sana. Nilijua kuwa kuna jambo zuri lingetokea kwangu leo. Unajua, ni kwa sababu nyota yangu ilisema hivyo.”

Yule mama akanijibu, "Sasa mpenzi wangu … kama Wakristo, sisi hatusomi nyota.” Hili lilikuwa ni somo langu la kwanza. Alisema kwamba Mungu alitaka kunipatia zawadi kwa kuwa sasa mimi ni Mkristo na akauliza kama ningependa kujua namna ya kuzipata zawadi hizo.

"Bila shaka ningependa," nilijibu huku akili yangu ikiwa inapiga picha ya boksi zuri lililofungwa kwa utepe. Kwa kweli sikujua alichokuwa anamaanisha. Lakini bado nilimpatia anwani yangu ili anitumie hiyo taarifa. Nilikata simu na kukaa kitandani huku nikitafakari yote yaliyonitokea.

“Hivi haya yalikuwa ya kweli? Ni nini hasa kilichotokea?” Mara moja Mungu aliniletea kumbukumbu za siku moja miaka miwili nyuma. Nikakumbuka kwamba nilikuwa nikimlilia Mungu kwa mateso huku nikiwa nimepiga magoti sakafuni nyumbani kwangu. Nikakumbuka kuwa niliinua mikono yangu kuelekea juu na kumwambia Mungu, “Hivi wewe kweli upo? Kwa nini basi hunijibu kama upo? Kwa nini maisha yangu yamejaa mateso kiasi hiki? Nataka wewe unijibu na si mtu mwingine yeyote maana siwezi kumwamini mtu mwingine yeyote tena! Nataka kukufuata wewe lakini sitaki kupoteza muda wangu kwenye dini isiyo ya kweli. Nataka kuwa na uhakika. Nijibu tafadhali. Nijibu!” 

Mungu alikuwa akinikumbusha kuhusu maswali yangu kwake kwa namna iliyo wazi sana. Ilikuwa ni kama skrini ya sinema mbele za macho yangu. Sasa nikajua kile ambacho kilitokea punde. Mungu yeye mwenyewe alinijibu kwa namna yake ya ajabu.

Sifahamu kama mwanga niliouona kwenye kile chumba siku ile ulikuwa ni kwa njia ya maono au ulikuwa ni mwanga wa kweli. Ila ninachojua ni kwamba, kile nilichoona na kusikia kilikuwa ni jambo halisi kabisa na kwamba hatimaye nilikuwa nimekutana na Mungu mmoja wa kweli kwa namna ya pekee sana. 

Siku iliyofuata nilienda tena kwenye maonyesho. Huko nyuma, nilikuwa nimepata Biblia ya buluu kwenye chumba cha hoteli ambayo ilikuwa inafanana kabisa na ile ya kahawia niliyoichukua kwenye chumba cha mwanzo. Huku kwa siri moyoni mwangu nikiwaza kwamba ile ya buluu itapendeza zaidi ikiwa chumbani mwangu, nilibadilisha zile Biblia; nikachukua ile ya buluu.

Akili yangu haikuwa kwenye kazi, bali kwenye Biblia na nilikuwa na shauku kubwa sana ya kuisoma kuliko nilivyowahi kufanya. Pale mume wangu alipoondoka tu kwenye banda letu, nilitoa ile Biblia yangu, huku nikiwa makini sana asije akaniona. Nikaanza kusoma kitabu cha Mwanzo. Ha! Nilikuwa nasoma Biblia ileile lakini sasa ilikuwa tofauti; ilikuwa na nguvu zaidi; na halisi zaidi! Niliipenda na nikaendelea kusoma hadi nikajisahau kwamba nilikuwa niko kazini. Ghafla nilisikia sauti ya mwanamume iliuliza,  "Unasoma nini?" Nikiwa nimegutuka, niliinua kichwa na kugundua kuwa kibandani kwetu kulikuwa na karibu dazani moja wa watu. Lakini ajabu ni kuwa sikumsikia hata mmoja wao akija. Kwa aibu, niliinua Biblia yangu kwa yule mwanamume na kumwonyesha maneno yaliyo kwenye jalada kisha nikaiweka chini Biblia ile. Ghafla nilijawa na aibu na woga pale nilipowaza, “Oh, kama baba yangu akiniona ninasoma Biblia atakasirika sana.” Kisha yule mwanamume akauliza tena kwa sauti huku akiwa na tabasamu pana, "Unasoma nini?"

“Hivi huyu mwanamume hajui kusoma?” niliwaza, “Ana tatizo gani?” Kama kwa hasira, nilijibu kwa sauti, “Biblia Takatifu!” 
Ghafla, watu wengine waliokuwa kwenye kibanda walianza kusema kwa sauti, mmoja baada ya mwingine:
"Utukufu kwa Mungu!"
"Amina!"
"Bwana Asifiwe!"
"Haleluya!"

Niligeuza uso kila upande huku nikitabasamu kwa watu hawa ambao walionekana kama vile wanang’aa kwa nuru na wenye furaha sana.

Nikamgeukia tena yule ambaye aliniuliza swali na nikamwuliza, "Nyie wote mko pamoja?"

"Hapana. Mimi niko hapa na mke wangu tu," alisema huku akitoa tabasamu pana. Huku nikiwa nimezidiwa na wingi huu wa wateja waliokuja ghafla, nikamwendea kila mmoja huku nikimwuliza kama alikuwa anahitaji nimsaidie. Hakuna aliyekuwa anahitaji msaada wowote, lakini kila mmoja alinitia moyo niende kuendelea kusoma Biblia yangu. Walikuwa wote Wakristo! Kisha mwanamume mwingine aliyesimama pembeni yangu alisema,  "Unaonekana kufurahia hicho unachokisoma."

"Ndiyo, ni kizuri sana. Je, wewe umewahi kusoma kitabu hiki. Kwa kweli unatakiwa kukisoma," nilisema.
"Ndiyo, nimeshakisoma kitabu hicho na ni kizuri sana," alijibu.
"Wewe ni Mkristo?" nikauliza.
Alitabasamu na kusema, "Ndiyo, mimi ni Mkristo."
"Aha," nilisema kwa aibu. "Je, uko pamoja na yeyote kati ya hawa Wakristo wengine?"
"Hapana," alisema.

Niliinuka kutoka kwenye kiti changu. "Unasema kweli? Naweza kukuuliza swali kuhusu Ukristo?" niliuliza.

Alinitazama huku akitabasamu. "Unajua,” alisema, “Naweza nikawa wa msaada kwa kuwa hiyo ndiyo kazi yangu. Mimi ni mtumishi na baba yangu ni mtumishi na babu yangu alikuwa mtumishi na mwanangu naye anasomea utumishi. Kwa hiyo, jisikie huru tu kuniuliza swali lolote kuhusu Biblia.”

“Aha,” nikasema, “Nina tatizo moja. Unajua, jana ndipo nilikubali kuwa Mkristo na nilichukua Biblia hii kutoka kwenye hoteli moja. Na sasa ninahofia kwamba Mungu atakuwa amenikasirika sana kwa wizi.”

Alicheka kisha akasema, “Umefanya vema sana kuwa Mkristo lakini hakuna tatizo kuhusu hiyo Biblia kwa sababu hiyo ni Biblia ya Wagidioni. Watu hawa hutengeneza Biblia na kuziweka kwenye vyumba vya mahoteli kwa ajili ya watu kama wewe. Kwanza, huwa wanafurahi wanapokuta Biblia imechukuliwa. Na Mungu naye anafurahia sana kwa kuwa unasoma Neno lake.”

Nilijawa na furaha sana kwamba ningeweza kubakia na ile Biblia.  Watu wote walipoondoka nilikuta kwamba nimefanya mauzo makubwa kwa saa ile kuliko nilivyowahi kufanya kwa siku nzima yoyote katika mwezi; na hayo yalitokea wakati nikisoma Neno la Mungu.

Kuanzia ziku ile sikuwa na hofu au aibu tena ya kusoma "Biblia Takatifu." Mungu aliwaleta Wakristo wote hawa ambao walikuwa hata hawajuani ili kunitia moyo. Je, hili lilitokea kwa bahati tu? Hapana! Ilikuwa ni kazi ya Mungu mwenyewe!  

Baada ya kurudi nyumbani California, nilipokea kile kijitabu kwa posta chenye taarifa za "Jinsi ya kuupokea zawadi kutoka kwa Mungu." Nilimkumbuka yule mwanamke wa kwenye simu siku nilipoamua kuwa Mkristo. Ilikuwa ni jioni na nilikuwa peke yangu chumbani. Nilifungua kile kijitabu na kuanza kusoma kuhusu “zawadi.” Zawadi ya kwanza iliitwa kunena kwa lugha. Ilisema kwamba, omba ili Bwana aguse kinywa chako kisha usubiri. Kwa hiyo, nilipiga magoti pembeni mwa kitanda changu na kumwomba Mungu. Kisha niliinuka, nikakaa kitandani, nikafunga macho yangu na kusubiri.

Baada ya kama dakika 2-3, midomo yangu ilianza kusogea na kuunda sauti "O" kisha sauti zingine na nikawa nazungumza maneno mbalimbali. Nilikuwa nazungumza lugha ambayo zikuwahi kuisikia maishani mwangu. Ilikuwa inafurahisha.

Nilitazama kijitabu tena na kusoma zawadi inayofuata kuwa ni "Tafsiri." Niliomba tena na nikapokea zawadi ile. Kisha ikafuatia “Unabii” na kadhalika kwenye orodha ile. Kufikia siku ya tatu, Mungu ambaye alikuwa mbali sana nami, akawa sasa ni rafiki yangu mkubwa duniani kote. Jambo la kwanza kabisa ninalokumbuka aliniambia ni kwamba alisema, "Amal, nakupenda." Nililia kwa siku 3 baada ya hapo kwa sababu nilikuwa najisikia sistahili upendo wake. Sikuelewa kwa nini Yesu afe kwa ajili yangu. Nilikuwa sikuzoea aina hii ya upendo.

Siku moja nikiwa katika maombi, nilimwuliza Mungu aniambie Roho Mtakatifu ni nani. Alinijibu kwa wazi kabisa, "1 Wakorintho 2: 12, 13, 14, 15, 16."
Nikasema, "Mungu, sielewi.”
Akarudia jibu lilelile na akaniambia nifungue Biblia yangu. Nilikuwa sijawahi kusikia neno “Wakorintho” kabla na nikawa najiuliza namba zile zote zinamaanisha nini. Lakini Mungu alinifahamu na alijua kuwa nitafungua sehemu ya yaliyomo. Mara nilipaona na hiki ndicho nilichosoma:  


12 Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.

13  Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni.

14  Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.

15  Lakini mtu wa rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu.

16  Maana, Ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo.


Baada ya kusoma hayo nikamwambia Bwana, "Una maana kuwa Roho Mtakatifu ni Mwalimu wangu?"
Nikasikia Bwana akijibu waziwazi, "Ndiyo."
Ah, nilijawa na furaha sana. Kisha nikauliza, "Roho Mtakatifu, una maana kwamba utanifundisha hii Biblia?"
Hapo tena nikasikia Bwana Mungu akisema, "Ndiyo."


Hisia za joto na furaha zilinijaa kiasi kwamba nilidhani nitapasuka. Unajua, nilikuwa siruhusiwi kwenda kanisani. Baba yangu ambaye alishaachana na mama alishanikataa. Kaka zangu walikuwa wanaona aibu kujihusisha na mimi na mume wangu naye alikuwa akinitesa kila siku. Nilikuwa na ndugu wa Kiislamu ambao walikuwa wakinipigia simu kila siku maana walikuwa wanataka kunifundisha Uislamu kwa uzuri zaidi. Lakini moyo wangu ulishaamua na hakuna ambaye angeniambia kuwa kile kilichonitokea hakikuwa cha kweli.

Mungu huzungumza nasi! Mungu mwenyewe alinitunza, na kila nilipokuwa na swali, aliniambia mahali pa kutazama kwenye Biblia. Mambo haya yaliendelea kwa miezi mitatu. Siku moja aliniambia nikabatizwe kwenye kanisa lililokuwa kwenye eneo letu. Kwa hiyo, kwenye siku ya kubatizwa, rafiki yangu "John", ndiyo, yuleyule tuliyekuwa naye kule Oklahoma, aliomba twende wote. Alisema kwamba hakuwahi kabla kushuhudia “Ubatizo wa Kikristo.” Wakati wa ubatizo, John alishikilia taulo yangu na Mchungaji alidhani kuwa naye alikuwa pale ili kubatizwa. John alimwambia Mchungaji kuwa, alipanga kuokoka kwanza wakati wa ibada. Nilishtuka sana kusikia kile kilichotoka kinywani mwa John. Kisha palepale aliongozwa sala ya toba na akabatizwa pia.

Nilifurahi sana kwa sababu rafiki yangu naye amempata Mungu. Hadi leo ninamwamini Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wangu. Na mbingu, ndiyo, nataka kuwa mbinguni pamoja na Yesu ambako nitamsifu rafiki yangu mkubwa kabisa kuliko wote duniani. Yeye ni Mungu Baba yangu na ni Yeye ndiye najitahidi kumpendeza leo.

Ilichukua miaka miwili kwa Mungu kunijibu na ulikuwa ni muda sahihi kwake.

Unaweza kuwa umemaliza kusoma ushuhuda huu sasa na huenda unajiuliza endapo haya ni mambo ya kweli. Ninakuhakikishia kwamba, nisingehangaika kupoteza muda wangu kuandika haya kama yasingekuwa ya kweli. Yesu Kristo ndiye jibu. Yeye ni Mungu!

Katika utumishi kwa Bwana wangu,
Amal.

***********************

Haya ndugu msomaji. Umemsikia dada huyu, Amal. Kwa nini usifanye kama alivyofanya yeye? Najua unayo shauku ya kwenda mbinguni baada ya hapa. Yesu peke yake ndiye njia ya kwenda mbinguni. Lakini wewe umefundishwa kwamba Yesu ni mtume tu na ni mwanadamu kama sisi na si Mungu wala si Mwana wa Mungu.

Hebu fanya kama Amal alivyofanya. Aliomba maombi ya kutoka ndani kabisa ya moyo wake. Alimwomba Mungu Muumba mbingu na nchi. Hiki ndicho alichomwabia Mungu:

“Hivi wewe kweli upo? Kwa nini basi hunijibu kama upo? Kwa nini maisha yangu yamejaa mateso kiasi hiki? Nataka wewe unijibu na si mtu mwingine yeyote maana siwezi kumwamini mtu mwingine yeyote tena! Nataka kukufuata wewe lakini sitaki kupoteza muda wangu kwenye dini isiyo ya kweli. Nataka kuwa na uhakika. Nijibu tafadhali. Nijibu!” 

Si lazima useme maneno hayohayo, lakini cha msingi ni kusema kile hasa ambacho moyo wako unakitaka. Wewe mwenyewe ni shahidi juu ya hali ya moyo wako katika jitihada zako zote za kujaribu kumpendeza Mungu. Nina uhakika kuwa hujafanikiwa hata kidogo. Nje ya Yesu ni maisha magumu, mazito, na yasiyo na tija. Sema naye leo. Mwambie Mungu mwenyewe akuthibitishie kama Yesu ndiye kweli njia ya kwenda mbinguni. Atakujibu!

Waweza pia kuusoma ushuhuda huu kwa Kiingereza kwa kubofya HAPA.


Pia unaweza kuwasiliana nami [blogger] kupitia:
Mungu akubariki.

No comments:

Post a Comment