Friday, December 28, 2012

Kuna Jambo la Ajabu Linaendelea Kwenye Ulimwengu wa Kiislamu




Takribani miaka 800 kabla ya Kristo, Mungu wa Israeli alisema kupitia nabii Yoeli kwamba:

Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono;

tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu.

Nami nitaonyesha mambo ya ajabu katika mbingu na katika dunia, damu, na moto, na minara ya moshi.

Jua litageuzwa kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla haijaja hiyo siku ya Bwana iliyo kuu na itishayo.

Na itakuwa ya kwamba mtu awaye yote atakayeliita jina la Bwana ataponywa; kwa kuwa katika mlima Sayuni na katika Yerusalemu watakuwako watu watakaookoka, kama Bwana alivyosema; na katika mabaki, hao awaitao Bwana. (Yoeli 2:28-32).

Jambo hili lilikuja kuanza mara baada ya Bwana Yesu kufufuka na kupaa kurudi mbinguni, pale Roho Mtakatifu aliposhuka kwa nguvu siku ya Pentekoste. Biblia inasema:

Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu … (Matendo 2:1-4).

Kwa sababu watu wote walipigwa na mshangao wa kile kilichokuwa kimetokea, Biblia inasema: Lakini Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu. Sivyo mnavyodhani; watu hawa hawakulewa, kwa maana ni saa tatu ya mchana; lakini jambo hili ni lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Yoeli, Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto.  (Matendo 2:14-17). Hicho ndicho kinachotokea kwenye ulimwengu wa Kiislamu sasa. Si kazi ya mwanadamu, bali ni Roho Mtakatifu mwenyewe yuko kazini!

Mbingu haziwezi kukaa kimya siku zote huku zikiona watu wakiwa wamefungiwa nyuma ya malango ya chuma. Nchi nyingi za Kiislamu ambazo zinaongozwa kwa sheria kali za Kiislamu zinapiga marufuku kabisa Injili ya Yesu kuhubiriwa kutokana na hofu ya watu kuuacha Uislamu endapo watajua upendo wa Mwokozi wao aliyewafia msalabani, yaani Yesu Kristo.

Hata baadhi ya watu ambao wanajitia nguvu kuingia katika nchi hizo  ili kuwapelekea watu Neno la uzima, wakikamatwa, wanafungwa au wanauawa – ama kwa kunyongwa, kuchinjwa shingoni, au kwa kupigwa risasi, n.k.

Lakini Neno la Kristo ambalo halipotei hata nukta moja hadi lote litimie, linasema kwamba: Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja. (Mathayo 24:14).

Dunia hii ni mali ya Yesu. Wanadamu wote ni mali ya Yesu. Mamlaka yote mbinguni na duniani amepewa Yeye. Mamlaka haya hayatokani na imani yetu. Tuamini au tusiamini, anayo tu! Ni Yeye ndiye aliyesema kuwa kabla hajarudi, INJILI NI LAZIMA IHUBIRIWE ULIMWENGUNI KOTE. Hii ina maana kuwa Injili ni lazima ihubiriwe Irani, Saudi Arabia, Uchina, Korea Kaskazini, Pakistani, Libya, Algeria, n.k. Huko kote wapo wana wa Ufalme ambao ni lazima wamkubali Yesu, maanatayari  wana nafasi zao kwa Baba mbinguni.

Wakuu wa dini na wakuu wa serikali wafanye kila watakalo, lakini Neno la Bwana Muumba wa mbingu na nchi halitanguki; halijawahi kushindwa na halitashindwa kamwe. Ni lazima litimie.  

Kwa sababu yule azuiaye ameweka mageti ya chuma na ngome za moto kwenye nchi nyingi ili Injili isihubiriwe, kuna jambo la ajabu linaloendelea kwenye ulimwengu wa Kiislamu hivi sasa. Mamilioni ya Waislamu wanakuja kwa Yesu – si kutokana krusedi na mikutano ya Injili – hapana! Ni kutokana na ndoto na maono kuhusu Mwokozi Yesu kama ambavyo Bwana aliahidi miaka mingi iliyopita kupitia nabii Yoeli.

Wakati watawala na polisi wao na magereza yao wakiwa wanazuia Injili kuhubiriwa, Bwana anawatembelea watu wake kupitia ndoto na maono. Makundi kwa makundi ya watu kwenye ulimwengu wa Kiislamu wanamwona Mwokozi kupitia ndoto na maono. Kupitia njia hizo, Bwana anajidhihirisha kwao, anasema nao, na matokeo yake wanampokea kama Bwana na Mwokozi wao PEKEE maana, zaidi ya jina la Yesu: hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. (matendo 4:12).

Enyi watawala mnaowafungia watu makongwa ya udini mtafanya nini sasa? Ninyi mnaowazuia watu wa Mungu kupokea uzima, si kwa sababu mnawatakia mema, bali ili tu muweze kulinda heshima za dini zenu, mtafanya nini sasa? Mtawekaje askari walinzi ndotoni sasa?

Hebu sikiliza ushuhuda kwenye video hapo juu ambao ni mmoja kati ya nyingi ambazo nitakuletea. Video hii inaonyesha kazi hiyo ya ajabu anayofanya Roho Mtakatifu kwenye ulimwengu wa Kiislamu hivi sasa.

Kwa kweli ndugu zangu Waislamu amkeni. Acheni kupenda dini kuliko kumpenda Mungu. Ukipenda dini, utaanza kulinda dini. Lakini ukimpenda Mungu, utalindwa na Yeye.

Video hiyo inaonyesha waumini wa Kikristo kule Kurdistan, Iraki ambao mwanzoni walikuwa Waislamu. Humo kuna wengi wanaoongea, akiwamo msimuliaji. Lakini mimi nitajikita zaidi kwenye maneno ya Wakurdistani wenyewe.

Mchungaji Zagros (mwenye nywele zilizochongoka mbele) anasema, “Biblia inatufanya tuamini kama kwamba Kitabu cha Matendo ya Mitume kitajirudia hapa Kurdistan.”

Baadaye anaendelea kusema, “Zamani nilikuwa mmoja wao kabla ya kuamini ujumbe kwamba ninatakiwa kuwaua wengine. Wakati mwingine nilitamani hata kumuua mke wangu kwa vile tu hajafunika kichwa chake. Lakini nilipoyapata maisha yangu ndani ya Yesu, kitabu cha Mathayo kinaniambia niwapende maadui zangu.”

Ukiendelea kusikiliza, hatimaye anaonekana dada mmoja anayesema, “Nina furaha sana kwa kuwa Yesu alikuja kugonga kwenye mlango wa moyo wangu. Ndipo nilipomjua Mungu wa kweli katika namna ya kweli ya maisha.”

Halafu anafuata baba mwingine mwenye kipara. Anasema, “Kabla sijawa muumini, siku zote nilihisi kuwa kuna kitu kimekosekana kwenye maisha yangu kana kwamba nimepoteza kitu. Hisia hizo ziliniandama kila wakati. Sasa hivi, baada ya kuwa mwamini, hisia hizo hazipo tena. Ninajua kuwa nimeshapata kile ambacho kilikuwa kinakosekana kwenye maisha yangu.”

Ndugu yangu uliye Mwislamu, je, wewe hufuatwi na hisia za namna hiyo? Je, si kweli kwamba kila wakati unajitahidi kumridhisha Mungu wako kwa mambo mengi kwa sababu ya ile hofu ya kutupwa jehanamu? Lakini si kweli kwamba hata ukijitahidi vipi bado unakuta hiyo hali ya kuhukumiwa inakuwapo moyoni? Kwa Yesu hakuna mambo kama hayo? Njoo upate amani ya kweli na wokovu wa kweli.

Kisha kwenye video anafuata bwana mwingine anayesema, “Watu wengi wanaona maono kuhusu Yesu; hata kama walikuwa hawajui chochote kuhusiana na Biblia au Agano Jipya au Kanisa. Wanamwona tu Yesu kwenye ndoto.”

Kisha Mchungaji Zagros anarudi tena na kusema, “Nilimwona Yesu kwenye ndoto mwaka 1999. Hakuniacha peke yangu. Alikuja tena. Alisema, ‘Nakupenda na ninataka uokoke.’”

Mchungaji Zagros anaendelea kusema, “Nataka kuuambia ulimwengu. Pokeeni upendo wa Mungu. Inaweza ikawa sasa au baadaye, lakini kila mmoja atakuja kupiga magoti mbele za Mungu. Ni bora kufanya hivyo sasa.”

Ndugu uliye Mwislamu, Yesu alikuja kwa ajili ya ulimwengu wote. Yesu hakuja kwa ajili ya Wakristo kama wengi wanavyodhani. Njoo kwa Yesu sasa upige magoti kwake maana Yeye ndiye Mungu wako aliyekuumba na kukufia msalabani kama sadaka ya dhambi zako na za ulimwengu wote. Unaweza kukataa kupiga magoti sasa kwa sababu huu ni wakati ambao tumepewa uhuru wa kuchagua. Lakini siku inakuja ambapo uhuru huo utaondolewa. Na hapo utapiga magoti tu! Ili si kwa kupenda, bali ni kwa lazima na baada ya hapo itafuata hukumu. Lakini nikuhakikishie kabisa kwamba Yesu anakupenda mno mno. Hata sasa analia kwa ajili yako. Anasikitikita kwa jinsi ambavyo hutaki wokovu wa bure na unakoelekea ni kubaya sana. Njoo leo!

Umeshaambiwa kuwa Yesu si Mungu, sawa; Yesu hakufa, sawa; Yesu ni mtume tu, sawa. Basi ninakupa changamoto. Najua unataka kwenda mbinguni. Pia najua kuwa kama ningekuwa na namna ya kukuonyesha kwa uhakika kabisa jinsi ambavyo Yesu ni Mungu, nina uhakika kuwa baada ya hapo, ungesema moja kwa moja, “Bwana Yesu nakupa moyo wangu.”

Si kwamba unamkataa Yesu kwa kuwa hutaki kwenda mbinguni, la hasha. Ila unamkataa Yesu kwa kuwa unaamini kabisa moyoni mwako kwamba hapo uliko, uko sahihi.

Basi ninakupa changamoto hii: MWITE YESU KWA MOYO WAKO WOTE NA UMWAMBIE KUWA AJIDHIHIRISHE KWAKO YEYE MWENYEWE!!

Kwani kuna ubaya gani? Huyo si ni binadamu tu kama unavyoamini? Kama ungekuwa unaamini kwamba Yesu ni jini, basi ungeweza kuniambia, ‘Sitamwita kwa kuwa atanidhuru.’ Lakini kwa vile unaamini kuwa Yeye ni mwanadamu tu; ni mtume tu, bila shaka hata akija, hatakudhuru kwa lolote. Basi mwite leo!!! Mwambie, “Yesu njoo ujidhihirishe kwangu.”

Roho Mtakatifu yuko kazini katika nyakati hizi za jioni ya ulimwengu huu; wakati ambapo tunamalizia majira na nyakati za ulimwengu huu. Mungu akubariki sana.

**********

Hata wewe uliye Mkristo lakini hutaki kupokea wokovu kwa sababu unasema, “Mimi sitaki kuitwa mlokole.” Ndugu yangu, dini– iwe ni Ukristo, Uislamu au dini nyingine yoyote – haina faida yoyote kwa mwanadamu. Yesu hakuja kuleta dini. Dini zilikuwapo tangu maelfu ya miaka kabla ya kuja kwa Yesu. Yesu alikuja kuleta WOKOVU kwa njia ya kujitoa sadaka ili, kwa imani na utii wetu kwa neno lake, tumpokee YEYE na si dini; maana Yesu ni NJIA, KWELI na UZIMA. Okoka leo!

No comments:

Post a Comment