Sunday, February 3, 2013

Muhubiri wa Kiislamu Kutoka Misri Aokoka Baada ya Yesu Kusema Naye Kupitia Ndotoni



Ibrahim alikuwa Mwislamu wa imani kali. Alikuwa mtoa mihadhara katika misikiti mbalimbali nchini Misri. Alikutana na Injili ya Yesu. Moyo wake ulitikiswa. Hakujua amwamini nani – je, ni Yesu au ni Muhammad? Nani angemwambia njia ya kweli ni ipi? Aliinua moyo wake juu mbinguni. “Yehova, nionyeshe njia ya kweli nami nitaifuata kwa gharama yoyote ile,” alisema kwa machozi.

Bwana Yesu mwenyewe alikuja kusema na Ibrahim katika ndoto. Ibrahim aliachana na Uislamu na kumkumbatia Mwokozi. Lakini kundi la Waislamu wenye imani kali la Muslim Brotherhood wangemwacha tu? Vipi kuhusu familia yake?

Kumfuata Kristo kuna gharama. Lakini huwezi kumbadilisha mtu anapomjua Mungu wa kweli ingawaje utampiga, utamfunga, na kumtesa kwa kila namna. Endelea kusoma ushuhuda huu wa kutia moyo na Mungu wa mbinguni atasema na moyo wako kwa njia ya ajabu ambayo itabadilisha kabisa maisha yako....!

Katika Bonde la Machozi

Mimi naitwa Ibrahim. Lakini kwa ajili ya usalama wa familia yangu, ninatumia pia jina la Timothy Abraham. Mimi ni Mmisri wa kawaida tu kutoka mkoa wa Delta. Nilizungukwa na mashamba kila upande, huku kukiwa na vijito vya Mto Naili. Nililelewa katika Uislamu thabiti wakati wa utoto wangu. Nilifundishwa kumwogopa Allah, ambaye aliumba mbingu na nchi kwa siku sita. Sikuwa na sababu hata moja ya kutilia shaka dini iliyosisitiza juu ya kumhofia Mungu, kutenda matendo mema na kuishi maisha safi. Kusema (reciting) Quran lilikuwa ni jambo lililotakiwa kuleta utulivu moyoni. Nilikuwa nafurahia ibada za Kisufi, maana wao wanamheshimu sana Muhammad. Hili lilikuwa ni kundi la Abu-al-Azayem. Nilikuwa natafuta kuwa na ukaribu zaidi na Allah.

Jioni moja kwenye saa moja hivi, katika msikiti wa al-Mahatta, nikiwa nimemaliza kuswali swala ya al-Maghrib, nilitambulishwa kwa Muhammad Imam na Sulleiman Kahwash. Hawa walikuwa ni watu waliotoa mchango mkubwa sana katika kuniingiza kwenye kundi lao, yaani The Muslim Brotherhood, au Udugu wa Kiislamu, au Al-Ikhwan al-Muslimin. Walinihimiza niwe Muislamu wa dhati kabisa na kufanya mfungo kila Jumatatu na Alhamisi na kufungua mfungo pamoja nao msikitini ambako tulikula mkate, siagi, tende (tamr), na saladi. Niliiga kwa juhudi kila kitu ambacho Mtume Muhammad alifanya, hata namna yake ya kukaa wakati alipokuwa akila. Hawa walikuwa watu wema sana kwangu. Pia, waliona kuwa mimi ninaweza kuja kuwa mzungumzaji mzuri sana. Kwa hiyo, Sulleiman Hashem, aliyekuwa kiongozi wakati huo, alinijia kwa upole na kusema, "Ibrahim, mafundisho ya Quran yanakuita ili utangaze ujumbe wa "da'awah" ya Uislamu.

"Allah wangu!" nilitafakari. "Mimi nina umri wa miaka 14 tu na ni mtu ninayeweza kutishika kirahisi."

Hata hivyo, Sulleiman alinipatia rundo la vitabu kwa ajili ya kusoma ili kujiandaa kutoa mhadhara siku iliyofuata. Kuanzia hapo, ikawa ni kawaida kwa mimi kufundisha siku ya Jumatatu ya kwanza ya kila mwezi. Nilikuwa nimejawa na ari kubwa kwani viongozi wangu walinifanyia mpango niende kwenye mji mwingine wa karibu, ili nikatoe mihadhara kwenye msikiti mmoja hadi mwingine. Kwa ari kubwa nilitaka kila mmoja afahamu utamaduni wa Mtume Muhammad, na matokeo yake, dada yangu hakuwa na uchaguzi isipokuwa kutii amri zangu zinazotokana na Quran za kuvaa mtandio kwa ajili ya kuonyesha staha.

Nilihitaji kuungwa mkono na baba yangu. Nilijiuliza iwapo alishawahi kumsikia mwanawe wa miaka 14, muhubiri wa Kiislamu. Kwa mshangao mkubwa, baba yangu alilaumiwa na watu kwa kuwa na mtoto ambaye sasa alikuwa wa imani kali. Udugu wa Kiislamu ulichukuliwa na Waislamu wengi wa kawaida kama ni genge tu la kidini.  Kwa hiyo, baba yangu akawa mkali sana kwangu na hata akanipiga ngumi mdomoni. Hivi sasa jino langu moja la mbele ni la bandia. Huwa linanikumbusha juu ya utayari niliokuwa nao hapo zamani wa kuteseka kwa ajili ya Uislamu mkali niliokuwa nao. Baba yangu aliteketeza maktaba yangu ya Kisuni (ambayo zaidi ilijaa vitabu vyenye mafundisho ya wahabi and salafi). Alijua fika kuwa Mohammad Mansour, polisi wa usalama mtoa habari (a security police informer), alikuwa akirekodi mafundisho yangu kutokea kwenye bafu la msikiti. Nilikuwa mkali sana kuhusiana na masuala ya sunnah ya Muhammad kiasi kwamba sikukubali kushikana mikono na wanawake. Nilichotaka tu mimi ni kuwa Mwislamu safi.

Baada ya kumaliza swala msikitini, baba yangu alimsimamisha mmoja wa viongozi wa kundi letu, Sulleiman Hashem, na akamsihi sana waachane na mimi. Baba yangu alipotoa kiapo cha talaka (hilif alaya bi al-talaaq) kwamba sitaruhusiwa kuingia msikitini ambamo watu wa Udugu wa Kiislamu wanaswali, nilimtii baba yangu, lakini nikamsihi aniruhusu nisikilize mafundisho yao kutokea nje ya msikiti.

Sikukatishwa tamaa na lolote kati ya haya na niliendelea kutoa mawaidha ya Kiislamu kila asubuhi (taboor as-sabah) na kwenye kila msikiti nilikoenda. Sikuwahi kuwaza hata kidogo kwamba Uislamu unaweza usiwe sahihi. Katika jitihada zangu za kueneza Uislamu kila mahali, siku moja nilikutana na gazeti moja ambalo lilikuwa na marafiki wa kalamu (pen pals) kutoka Marekani. Nilimchagua mmoja na kumwandikia barua, nikitarajia kumfanya awe Mwislamu siku moja. Niliandikiana barua na John kutoka Pennsylvania, Marekani kwa muda wa miaka miwili, huku kila mmoja akijaribu kumfanya mwenzake aingie kwenye dini yake. Nilisoma kila kitabu nilichoweza kukipata ili niweze kupinga mafundisho ya Biblia. Mbaya zaidi, sikuwa na heshima kwa Biblia maana niliweka miguu na viatu vyangu juu yake; kwa kuwa Quran ilinifundisha kwamba kitabu hiki kimepotoshwa na wanadamu.

Kisha, kwa mshangao wangu, John alikuja kunitembelea kijijini kwangu. Hiyo ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kumwona Mkristo halisi. Ukweli, uwazi na uhalisi wake vilinigusa sana. John alikaa nami kwa miezi miwili. Alikuwa na maisha ya maombi ya kushangaza sana ambayo yalikuja kuwa mwongozo wangu hapo baadaye. Sikujua kuwa Wakristo huomba hadi pale nilipokutana na "barua iliyo hai" katikati ya nyumba yangu, mtu aliyetoka mbali na kuja kuwa mmoja wetu na akaonyesha wazi upendo wa Kristo. John alikuwa na maisha ya ajabu ya maombi maana aliomba zaidi kuliko kuzungumza, huku akisema maneno ya kwenye Biblia. Nilianza kuonea wivu ukaribu na Mungu aliokuwa nao John, kisha nami nikaongeza bidii katika kusema (recite) Quran.

Uislamu ni dini ambayo inahitaji kupewa sifa ya kuwafundisha wafuasi wake kuwa wema, wasafi na wakarimu. Hakuna shaka kwamba Muhammad anabakia kuwa ni mtu mwenye kipaji katika historia. Na jambo jingine la kukumbuka ni kuwa Mwislamu anaweza kufanya matendo mengi mema kadiri awezavyo katika dunia hii, lakini katika Siku ya Hukumu, Mungu atayapima matendo ya kila mtu kwenye “mizani". Matendo mema yatawekwa upande mmoja na matendo maovu upande mwingine. Kama matendo mema yakiwa mazito kuliko matendo maovu, basi muumini huyo ataingia peponi, ambapo Quran inasema ni mahali penye raha ya kufanya ngono  na kuchezacheza na wanawake wenye macho makubwa (sura al-Waqia 56:20-23). Hata hivyo, Kristo Bwana wetu alisema kuwa "Kwa maana katika kiyama hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika mbinguni.” (Mathayo 22:30).

Rafiki yangu Mwislamu, kulingana na Uislamu, kama matendo yako maovu yatakuwa ni mazito kuliko matendo mema, utatupwa jehanamu ya moto. Inaonekana kwamba utatakiwa kuwa na wema wa asilimia 51 tu ili uweze kuingia peponi. Lakini bado unabakia huna uhakika endapo utaenda peponi. Kile unachosema tu, wewe rafiki yangu Mwislamu ni “Mungu tu ndiye ajuaye.” Unatumainia rehema za Allah na kutumaini kuwa malaika au Mtume wataingilia kati kwa ajili yako katika siku ya mwisho, ili uweze kupona jehanamu ya moto.

Mimi nami nilikuwa kama wewe, dada na kaka yangu Mwislamu, ndani ya meli hiyohiyo, hadi pale nilipokuja kutambua kuwa kumbe mtu anaweza kujua kwa uhakika kuwa anakwenda mbinguni. Huwa ninabubujikwa na machozi kila ninapotafakari jinsi nilivyokuwa nimepotea na sasa nimepatikana. Nikiwa ninatetemeka kwa machozi, na kuona  utukufu wa Mungu, ninashangilia kwa furaha kujua kuwa ninao uzima wa milele kwa hakika.

Mungu wa Biblia ni wa haki na pia mwenye rehema. Haki yake inataka kila mmoja atupwe jehanamu, maana Yeye ni mkamilifu kwa asilimia 100. Hata tukijitahidi kwa kiasi gani kumpendeza Mungu, kamwe hatuwezi kufikia ukamilifu wake. Matendo yetu mema hayawezi kamwe kutuleta karibu na Mungu. Mungu aliona jinsi tulivyopungukiwa, akaamua kulipa Yeye mwenyewe adhabu iliyotustahili sisi.  Alituma Neno lake, Isa Al Masih (Yesu Kristo), ambaye hana kabisa dhambi au upungufu wowote, akaja akabeba dhambi zetu msalabani. Utamwambia nini Jaji pale anapoamua kulipa adhabu yako? Biblia inasema katika Yohana 3:16: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

Ni kwa sababu Mungu anatupenda ndiyo maana alimtuma Neno, Yesu Kristo, kuja kufa kwa ajili yetu. Uislamu kamwe hautupi uhakika wa kwamba tunaenda mbinguni, lakini Kristo anafanya hivyo! Mungu asifiwe! Asante, Bwana wangu, kwa kuamua kulipa gharama iliyotakiwa Wewe mwenyewe kupitia Neno lako lililofanyika mwili, yaani Bwana Yesu Kristo, ambaye ni ufunuo kamili wa namna Mungu alivyo.

Baada ya John kuondoka, ushawishi wake ulibakia. Nilidhani kuwa nitamhuzunisha John kwa kusema, "John, kunitembelea kwako kumenifanya niwe Mwislamu imara zaidi kiimani, hivyo usijisumbue tena kuwabadilisha Waislamu.” Lakini badala yake John alishinda katika sala na maombi yake. Maombezi yake yalimfanya BWANA aniamshe katikati ya usiku maana sikuwa na usingizi au pumziko. Hali ya kukosa amani ndani yangu ilifikia upeo wake wa juu. Nikiwa katika hali hiyo, nilichukua Biblia na kuifungua tu bila kujali itafungukia wapi. Nilipofungua, nikakumbana na maneno:  "Sauli, Sauli, mbona waniudhi?"

Nakumbuka siku moja tukiwa na mjadala mkali na John. Nilidhihaki Biblia na kusema,  "John, Biblia yenu ni moja kati ya vitu vya kipuuzi kabisa! Unawezaje kuamini hadithi ya Sauli aliyekuja kuwa Paulo, mtumishi wa Injili?”
John akasema, "Hadithi hiyo ni ya kweli, na ndiyo maana nina uvumilivu juu yako. Siku moja utakuwa Paulo mwingine!”
Nikajibu, "John, utakuwa na wazimu kufikiria hata sekunde moja kuwa ninaweza kuacha dini ya dini zote, Uislamu!”

Nikiwa sasa natafakari juu ya ‘Sauli, Sauli ...’ nikasema, “Bwana! Mimi? Nakuudhi Wewe? Sijakufanyia chochote kibinafsi ... Nakumbuka nilienda kumshitaki polisi mwanafunzi mmoja wa kike wa udaktari ... lakini Wewe binafsi sijakufanyia lolote baya. Je, ni kweli kwamba amgusaye yeyote kati ya watu wako anagusa mboni ya jicho lako?”

Uislamu unakana kusulubiwa kwa Bwana Yesu Kristo kwa sababu Quran ilitaka kuwanyima Wayahudi ushindi waliosema kuwa wanao ndani ya kifo cha Yesu.  Quran inatamka kwamba Mungu alimweka msalabani mtu mwingine aliyeonekana kama Yesu. Sasa rafiki zangu Waislamu, Mungu hayuko kufanya kazi ya udanganyifu. Maana, kama alitaka kumwokoa Yesu kutoka kwenye msalaba, angeweza kufanya muujiza bila kutumia uongo na udanganyifu wa kuweka mtu anayefanana na Yesu wakati si Yesu.

Kosa hili la Quran liko wazi na linadhihirisha kuwa Quran haitoki kwa Mungu wa kweli. Zaidi ya hapo, Quran inajipinga yenyewe, maana ingawaje inasema kwamba Wayahudi hawakumuua Yesu, inathibitisha wazi kabisa uhalisia wa kifo cha Yesu katika sura Imran (3):55 pale Allah anaposema katika sehemu ya kwanza ya aya hiyo kuwa:

"Oh Jesus, I shall cause you to die,
and then I shall raise you up to me."

Yaani:
“Ewe Yesu, ninaenda kusababisha ufe,
kisha nitakufufua uje huku kwangu.”

Rafiki yangu Mwislamu, lengo langu hapa si kukufanya ubadili dini yako, bali ni kukufanya ujiulize swali kuu: Yesu ni nani? Je, alisulubiwa? Na je, jambo hili lina athari gani kwako?

Kama historia nzima ya mwanadamu inahusiana na Kristo, basi maisha yangu yote na uwepo wangu vinatakiwa kuhusiana naye vilevile. Kuukana msalaba wa Kristo ni kuikana historia yenyewe. Muhammad mwenyewe anatajwa kwenye Quran kuwa aliambiwa na Allah kwamba awe anarejea kwa Watu wa Kitabu (Wayahudi na Wakristo) kama ana shaka na Quran:

"And if thou (Muhammad) art in doubt concerning that which we reveal unto thee, then ask those who read the Scripture (that was) before thee." Sura Yunus 10:95

Yaani:
“Endapo wewe (Muhammad) una shaka yoyote kuhusiana na kile tulichokufunulia, basi waulize wale waliosoma kitabu kabla yako.”

Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilianza kujiuliza swali “Kwa nini?” na nikahoji kila kitu ambacho sikuwa nakitilia maanani hapo kabla. Nilichunguza kila dai kwa undani kabisa. Jambo hili lilinisababishia matatizo kwenye jamii iliyoongozwa kwa utii wa kulazimishana. Wao wanasema kuwa maswali yanaruka hadi kwenye uso wa Allah. Wewe tii tu. Basi! Ndani ya Udugu wa Kiislamu, wito (motto) wetu ulikuwa ni: "Samaana wa ataana", yaani "Tumesikia na kutii."

Baada ya miaka kadhaa ya kujifunza, nilifikia maamuzi mawili yenye mantiki: Biblia ni Neno la Mungu lisilo na makosa, na Yesu ni Neno la Mungu. Nilianza kuona kuwa ilikuwa inawezekana kwa Yesu kuwa Mungu. Kwa akili, nilikubaliana na madai yote ya imani ya Kikristo. Lakini moyoni bado nilikuwa nina hofu ya kupigwa na kufa iwapo nitamwita Mungu Mwenyezi “Baba yangu!” Nilihitaji muujiza! Biblia inatufundisha kuwa hakuna mtu anayeweza kusema: “Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu” (1 Wakorintho 12:3).

Haishangazi basi kwamba kila tukio la Wokovu ni muujiza wa kuzaliwa kutoka kwenye mauti na kuingia kwenye uzima wa milele!  

Kutokea ndani kabisa ya moyo wangu, katikati ya mabishano ya ndani yangu, nilimlilia Allah, hata ndani ya msikiti, nikisema, "Bwana, nionyeshe ukweli! Je, ni Yesu au ni Muhammad? Hivi inawezekana Wewe ukawa ni Baba yangu? Nionyeshe ukweli. Na ile kweli utakayonionyesha, nitaitumikia maisha yangu yote hata iwe ni kwa gharama gani!”

Nilibubujikwa na machozi maana nilijua kuwa gharama inaweza kuwa ni kubwa sana kwa mtu dhaifu kama mimi. Maana nitawezaje kukabiliana na hali ya kukataliwa na familia yangu, halafu nikalale mitaani kama mtu asiye na kwao? Na itakuwa vipi pale viongozi wangu kwenye Udugu wa Kiislamu watakapojua? Na vipi kama, katika ari iliyo katika Uislamu wao,  wataamua kuulinda Uislamu huo kwa kuniua mimi?

Kulingana na dini ya Kiislamu, mtu anayeacha Uislamu anatakiwa kupewa siku tatu za kuurudia. Akikataa basi ni halali kumwaga damu ya muasi huyo kwa jina la Allah!

Maneno ya Mtume Muhammad yaliendelea kujirudiarudia masikioni mwangu: "Mtu yeyote (yaani Mwislamu) ambaye amebadili dini yake, muueni.” Utamaduni huu umesimuliwa na Abu Bakr, Uthman, Ali, Muadh ibn Jabal, na Khalid ibn Walid. Hata hivyo, nilizidi kumwomba Mungu aniongoze. Niongoze, Ee Yehova Mkuu, uje kwenye nchi hii kame; mimi ni dhaifu, lakini Wewe unazo nguvu.

Usiku mmoja Kristo alinitokea kwenye ndoto na akasema nami kwa sauti tamu ya upole, “Ninakupenda!” Niliona jinsi ambavyo nilipingana naye kwa ukaidi kwa miaka hii yote. Nami nikamwambia katikati ya machozi, "Nakupenda pia! Ninakujua! Wewe ni wa milele na milele!” Mara niliamka usingizini huku uso umefunikwa na machozi, lakini nikiwa nimejawa na furaha tele. Niliamini kuwa Kristo mwenyewe amenigusa akili na moyo wangu. Nikamkubali!

Kuanzia hapo, nikajawa na ari kubwa sana kwa ajili ya Kristo. Nikarukaruka, nikaimba, nikasifu Jina lake na nikawa nasema naye usiku na mchana. Nikawa hata nalala na Neno la Mungu lisilo na makosa, yaani Biblia, karibu na kifua changu.  

Nilipitia uzoefu wa "mtoto aliyeharibika" (spoiled child) wa Mungu anavyokuwa: yaani Mungu alikuwa akinipatia kila kitu nilichomwomba katika sala. Lakini sasa Bwana alitaka nimpende na kumwabudu Yeye kama Yeye, na si kutokana na yale aliyokuwa ananipatia. Nilijitahidi kuifanya imani yangu kuwa siri, hivyo nilibatizwa kwa siri kwenye nyumba ya mchungaji.

Nikiwa nimejawa na furaha ya wokovu, sikuweza tena kumficha au kumkana Kristo. Kwa hiyo, pale rafiki yangu mmoja wa utotoni aliponiuliza iwapo Kristo alisulubiwa, nilijibu, “Ndiyo!” na nikamweleza ni kwa nini. Aliomba pamoja nami ili kumpokea Kristo. Kila mara tulipoomba pamoja alikuwa akitikisika na kutokwa na jasho. Aliweza kuona jinsi Jina la Bwana Yesu lilivyo na nguvu.  Viongozi wangu wa zamani katika kundi la imani kali la Kiislamu, wakitaka kujua nani aliyemhubiria huyo rafiki yangu. Walimtishia kuwa wangemuua kama asingewaeleza kila kitu kuhusiana na uenezaji wangu wa Injili.

Cha kusikitisha, alinisaliti na matokeo yake nilipigwa mbele ya msikiti ambako zamani niliwahi kutoa mihadhara ya kiislamu kwa ari kubwa. Kwa upande wao, mimi nilikuwa kafiri aliyestahili kuuawa isipokuwa kama ningeamua kuirudia dini yangu ya zamani. Waliona kuacha kwangu Uislamu kama ni aina mbaya zaidi ya kuasi Uislamu na Quran. 

Kwa kuwa kubadili kwangu dini sasa kulikuwa kunajulikana na kila mtu na Waislamu wakawa wanapanga kuniua, ilinibidi nikimbie. Niliwindwa na Waislamu kutoka kwenye kijiji changu kule Delta, mpaka Ismailia hadi nilipofika Kairo, mahali walikoishi rafiki zangu wa Kikristo. Lakini pamoja na hayo, rafiki zangu hao hawakuwa tayari kunihifadhi. Ikanibidi nirudi tena kijijini na nikajiachilia kwenye mikono ya Mungu ilindayo.  

Niliporudi nikitokea Kairo, nilikuta kundi lenye hasira la Waislamu limejaa kwenye nyumba yetu. Mama yangu alikuwa amevaa mavazi ya msiba, nguo nyeusi kama ilivyo utamaduni wa Misri. Kwao, kitendo cha mimi kuuacha Uislamu, nilikuwa nimekufa!!! Wanawake wa Kiislamu walinipigia kelele wakisema, “Mama yako hastahili yote haya kutoka kwako. Kwa nini umsababishie majonzi yote haya?” Mwanamke mwingine naye akasema, “Maskini mama wa watu! Mwanawe amemwacha ili akaungane na makafiri wa Kikristo. Kama ningekuwa yeye, ningemuua mtoto huyo kwa kuwakimbilia makafiri kama mbwa.”

Nilipokea barua kutoka kwa rafiki yangu wa Jodani akisema kuwa baba yangu alikuwa akitembea barabarani huku akilia kwa uchungu kutokana na vibarua wa Kiislamu wa kule kumsuta  sana uhusiana na suala langu. Aliugua na kulala kitandani kwa mwezi mzima kwa sababu ya mambo haya hadi pale alipozungumza nami kwa simu.

Sitasahau kamwe jinsi Waislamu wenye hasira walivyokuja kuvamia nyumba yetu kikatili sana. Mama yangu alipiga magoti mbele ya jirani yetu, "Sayed" akimsihi wamuue yeye badala ya kuniua mimi. Katikati ya mateso makubwa namna hiyo, mama yangu alinikana na kunikataa mbele ya watu wote kijijini kwetu. Nampenda sana mama yangu kuliko mtu yeyote duniani, lakini hakuna nguvu yoyote ya kibinadamu, hata kama ni kubwa kiasi gani, inayoweza kunitenga mimi na upendo wa Kristo. Daima nitaishi kwa ajili ya Yesu.

Biblia yangu, vitabu vyangu vyote vya Kikristo, na kanda za nyimbo vilitwaliwa na kuchomwa moto. Niliamua kukimbia kutoka Delta hadi Kairo. Japokuwa polisi walikuwa wananifuatilia, Bwana aliwapiga upofu na kunilinda. Nikiwa Kairo, nilijificha kwa M, rafiki wa Kimisri wa Kibaptisti aliyekuwa akinifariji muda wote. Nilitokwa na machozi pale aliponisomea maneno haya: 
"Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo” (Matendo 5:41)

Namshukuru Mungu kwa kunipatia rafiki huyu, M., ambaye alinifundisha jinsi ya kuishi maisha ya ushindi, ibada na shukurani. Alinipatia Biblia ndogo ya mfukoni (Agano Jipya kwa Kiarabu) na akaniambia wazi kwamba wazazi wake walikuwa wana wasiwasi. Pia niliambiwa kuwa, kama wakiendelea kunificha pale, wangeweza kufungwa maisha kama wangekamtwa. Sikuwa na mahali pa kwenda.

Kwa hiyo, kutokana na ushauri wa mchungaji wangu wa siri, nilirudi tena kijijini kwangu, huku nikiwa nimeficha Biblia yangu ya Kiarabu kwenye soksi, na kuomba Mungu kwamba isionekane kwa yeyote.

Matokeo yake niliweza kukamatwa na kuachiwa tena na tena. Nilijifunza nini maana ya Mungu kuwa sehemu yangu pekee ya kujificha. Gerezani, Mwokozi wangu anajua kuwa nimekuja kupata amani ya kweli. Sikutetereshwa kwa sababu nilimwona Kristo gerezani; sikujiona mimi. Niliimba nyimbo za furaha katikati ya machozi, huku nikitarajia Nyota ya Asubuhi aje na kuniokoa. Niliamua kuificha Biblia mahali ambako polisi hawangeweza kuiona na kuichukua – yaani moyoni mwangu kwa kuikariri. Tangu wakati ule imekuwa ni kawaida yangu kulala na Biblia yangu pembeni mwangu.

Miaka mitano baadaye, nilifanikiwa kutoroka juhudi za Waislamu kutaka kuniua na nilishituka sana kugundua kuwa kule Marekani wapo Wakristo wanaoishambulia Biblia ambayo mimi nilikuwa tayari kufa kwa ajili yake. Neno la Mungu limenipatia ahadi za imani ambazo ninazitumia kama mtoto mdogo na kuomba kupitia hizo kwa kujiamini kabisa. Malango ya Mbinguni yanafunguka pale tunapoomba kupitia Neno la Mungu. Neno lake linaongea uzima!!!

Wakati fulani nilipoenda kumpelekea mama yangu zawadi ya Siku ya akina mama, aliniuliza, “Zawadi ya siku ya akina mama?”
Nikajibu, “Ndiyo” kila aliporudia swali lile. Alinitazama kwa uso wenye huzuni kubwa sana na kusema, "Mwanangu ambaye nilimngoja kwa miaka 15 ili kumpata na baadaye akazaliwa, hivi sasa alishakufa. Ninakukataa hadi siku ya hukumu, Ibrahim." Nililia lakini Kristo aligusa moyo wangu na kusema, “Mimi ni familia yako sasa! Mimi ni baba, kaka, mama, dada, rafiki na kila kitu kwako sasa, Timothy."

Sitasahau siku zile pale ambapo mama yangu angewaita polisi ili waje kunikamata. Alienda hata kwa mchawi ili wanitupie uchawi na kunirudisha kwenye Uislamu.  Yule mchawi alisema, "Mwanao anafuata njia ambayo kamwe hataiacha na atakuwa mshindi katika maisha yake yote kama tu ataendelea kubakia kwenye njia hiyo.”

Maneno haya, kutoka kwenye kinywa cha mchawi, yalimfanya mdogo wangu aje kwa Kristo. Ushuhuda wa mapepo juu ya ushindi wa Bwana wetu hufanya hali ya kushuku na kukosa imani zionekane kuwa ni upuuzi (Tafadhali soma Warumi 8:35-39). Unaweza nawe pia ukawa zaidi ya mshindi kupitia Kristo, Mshindaji wako ambaye anakupenda! Amini hilo!

Nilipoteza Biblia yangu na vitabu vyangu vyote vya Kikristo baada ya kunyang’anywa. Nilichobakia nacho ni redio tu. Nilikuwa najificha mahali na kusikiliza kwa siri idhaa ya Voice of Hope, ili kuweza kusikia nyimbo za faraja wakati wa usiku. Lakini mama yangu alinikamata na mara moja alinipokonya ile redio na akanipiga kichwani kwa viatu vyake. Nilikuwa na umri wa miaka 20 wakati ule. (Ningependa ujue pia kuwa hivi sasa mimi huwa naongea waziwazi kwenye Voice of Hope maana ninaishi kwenye nchi iliyo na uhuru, Amerika).

Niliomba kwa ajili ya Biblia na Bwana akanijibu. Nilienda kuchukua kifurushi cha Biblia  kutoka posta. Mkuu wa posta, Kamal, alinipiga kofi kwa nguvu na kunipiga ngumi usoni. Nilikutana na kila aina ya vitisho ... nilikuwa nalia kutokana na maumivu. Aliniambia, "Wewe nenda tu kwa hawa makafiri Wakristo, nasi tutakutowesha mara moja. Tutakupeleka nyuma ya jua!"

Hatimaye, nilijisikia kuomba ili niondoke Misri niende nikaishi imani yangu kwa Kristo sehemu nyingine. “Baba wa faraja,  haujawahi kuniacha. Tafadhali, unikumbushe juu ya Mwanao aliyening’inia msalabani huku akilia kwa maumivu makali sana akisema, ‘Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?’ Bwana Yesu, wote walikukimbia, lakini bado ulipata pumziko kwa Baba. Nahitaji nami kumtegemea Baba kama ulivyofanya Wewe.”

Baada ya miaka 3, niliamua kuhamia Kairo ambako nako hakukuwa salama. Mara ya mwisho polisi waliponikamata walisema,  "Kulingana na sisi, wewe ni kafiri ulitenda kosa kubwa sana. Mara nyingine tutakapokukamata tena, utapata adhabu ya kifo.” Mbaya zaidi, mwenye nyumba ambaye alikuwa ‘Mkristo’, alisema kuwa hawezi tena kumhifadhi mhalifu mtoro.

Sikuwa natakiwa kwenye nchi yangu mwenyewe. Hata hivyo, Bwana aliingilia kati, na mwinjilisti mmoja wa Kipalestina,  Anis Shorrosh, alinitambulisha kwa Dk. Paige Patterson. Huyu alianza kuniongoza jinsi ya kuomba viza kwenda Marekani. Mara ya kwanza nilinyimwa, lakini Dk. Patterson hakukata tamaa. Hatimaye, niliweza kupatiwa viza, na kimiujiza, niliweza kuondoka Misri. Bwana, Wewe huwa hauokoi wanao kutoka utumwani ili baadaye uje kuwarudisha tena ... Nisaidie niweze kwenda mahali ambako ninaweza kuishi imani yangu ya Kikristo bila ya kunyanyaswa na polisi. Bwana, tafadhali fanya kila liwezekanalo ili nisilazimike kuishi mahali ambako watu watanilazimisha kwenda msikitini. Wewe unataka wanao wakuabudu kwa uhuru hata kama hii inamaanisha kukimbia kuponya maisha yao kama mimi ili kwamba Kristo aweze kuwa yote katika yote.  

Kama asingekuwa Dk. Patterson, hivi sasa ningeshakuwa historia. Nilikuwa nimepangiwa kuuawa, na Mungu akaona kuwa bado alikuwa na kazi ya mimi kufanya. Kwa hiyo, alimtumia Dk. Patterson kimiujiza kuokoa maisha yangu. Mungu Mwenyezi ni Baba wa wasio na baba (Zaburi 68:5), na baba na mama yangu wakiniacha, kama anavyosema Daudi, BWANA ananishikilia kwake. Je, Mungu Mwenyezi, ni Baba yako ewe rafiki yangu? (Wagalatia 4:6). Mungu Mwenyezi anakupenda wewe kibinafsi (Mithali 8:31).

Baada ya kukimbilia Marekani, bado nilikuwa nina hofu kuwa iko siku nitakabiliana tena na polisi wa Misri, hasa ukichukulia kuwa nilikuja huku kwa viza ya uanafunzi, ambayo ingeisha muda wake siku yoyote. Kulingana na serikali ya Misri, mimi ni kafiri ambaye nimeukashifu Uislamu na pia kuharibu umoja wa kitaifa. Allah peke yake ndiye anayejua kuwa sina kinyongo chochote na Misri, nchi nilikozaliwa, au na Uislamu. Wahubiri walikubali kunificha kwenye mashamba ya mifugo, kama mambo yangefikia kubaya. Nilitaka tu kuishi na nisiwe sababu ya ghadhabu za kidini za mtu yeyote.

Shirika moja lilinifadhili na kuniombea ukaazi wa kudumu. Baada ya kusubiri kwa miaka sita, Bwana alijibu maombi yangu. Nilipata ukaazi wa kudumu, siku chache kabla ya harusi yangu, Aprili 18, 1998. Sikutaka mtu yeyote anituhumu kuwa nimeoa mke ili niweze kupata kibali (green card). Nilimwoa Angela kama yeye tu na si kwa lengo la kupata hicho kibali. Ninajitoa kwa Angela kila kitu changu, maana chanzo cha pendo letu ni Mungu. Si jambo la hisia za mpito tu, bali ni agano ambalo BWANA ni Shahidi kati yangu na mke wa ujana wangu, mwenzi wangu na rafiki yangu mkubwa. (Malaki 2:14).

Hapa ni wakati wa mimi kumsifu Mungu kwa zawadi ya ndoa. Ni pale nilipojiachilia kwa Mungu na shauku ya kiungu ya kuoa ndipo aliponiletea Angela. Angela ni malaika wa Mungu kwa ajili ya moyo wangu. Ni mzuri ndani na nje pia. Sote tuna mtazamo mmoja juu ya kudhihirisha upendo wa Kristo kwa kaka na dada zetu wa Kiislamu. Sikutaka pungufu ya kile ambacho nilijua Allah alitaka nikipate: Angela ni mwanamke wa maombi, mwenye kujali na mwenye upendo, mkarimu, mtoaji na mwenye kupenda ushirikiano. Ni mkamilifu kwa ajili yangu. Ninafurahia kwamba anawapenda wazazi wangu na anajitoa sana kwao. Bwana, ni nini nilichotenda hadi kustahili wema mkuu namna hii kutoka kwako, hadi unipe mke anayenipenda mimi pamoja na familia yangu? Bwana aliniheshimu kwa kumweka Yeye juu ya shauku yangu ya kupata mke, na sasa sisi ni wenza waombaji. Hakika Muumba na Mkombozi wetu anajua kuwakutanisha watu wanaoendana.

Bwana, nisaidie nisije kuwa na amani katika lolote kama litasababisha kupoteza ushirika wangu nawe. Je, si Wewe uliyetuambia kwamba: “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka” (Marko 13:13)?

Tafadhali, usiniache nikaharakisha wokovu wako, Bwana, katikati ya magumu. Lakini, tafadhali, nipe uvumilivu ili niweze kustahimili magumu kama askari wa msalaba wa Kristo! Bwana, nifunike kwa pendo lako kiasi kwamba, kufanya mapenzi yako kuwe ni mkate halisi katika maisha yangu. Katika jina la Kristo, amen!

Rafiki zangu, jisikieni huru kuwasiliana nami kupitia baruapepe hapa.

[Angalizo la blogger: Kama unapenda kuwasiliana na Ibrahim, fanya hivyo kwa lugha ya Kiingereza, si Kiswahili. Maana ushuhuda huu ni tafsiri kutoka Kiingereza. Unaweza kusoma ushuhuda huu kwa Kiingereza kwa kubofya HAPA.]

24 comments:

  1. conglatulation Ibrahim

    ReplyDelete
  2. Daa lakini ndugu zangu waislam mnashindwa vipi kuwapa ukweli waumini wenu juu ya uongo na uovu wa dini yenu? kuweni wawazi mtaweza vipi kumfuata mtume wenu aliye motoni? tafadhalini njooni kwa YESU muachane na majini.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Ndugu yangu. Asante kwa maoni yako. Lakini si kazi rahisi hata kidogo kwa mwislamu kuacha dini hiyo na kuingia kwenye Ukristo kama ambavyo si rahisi kwako uliye Mkristo kuingia kwenye Uislamu. Hii ni kwa sababu nao wanaamini kwa kaiwango kilekile tunachoamini sisi kwamba wako sahihi.

      Kwa hiyo, shida haiko kwenye kuamini bali ni kwenye KUTAMBUA kuwa unachokiamini si sahihi.

      Ni Roho Mtakatifu pekee kupitia maombi yetu ndiye anayeweza kufungua fahamu zao ili, kama isemavyo Biblia, NURU YA INJILI IWAZUKIE.

      Hili si jambo rahisi kibinadamu. Ndiyo maana hata ukija ndani ya Ukristo wenyewe, wengi wanakataa wokovu na kung'ang'ania dini. Ni yaleyale!

      Bwana akubariki.

      Delete
  3. Kwanza kabisa napenda kumpongeza Timothy kwa ushuhuda wake ukweli umenitoa machozi ni jinsi gani Yesu alivyomnyenyekevu na wa haki, Unjajua ni nini kaka Anonymous wanashindwa kumtambua Yesu na kuacha majini kwa sababu hawana Roho Mtakatifu hivyo me nadhani tuwaombee tuu na kuwapenda naamini iko siku watatokewa tuu na huyu mwanaume Yesu. Dah!!!!!!! kwa dizaini hii basi hata sisi tupate changamoto kumtafuta yeye kwa bidii.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Kama ilivyokuwa vigumu SANA kwa watu wa wakati wa Yesu kuamini kuwa alikuwa ni Mungu, maana walimwona akizaliwa na kukua kama watoto wengine, ndivyo ilivyo vigumu sana kwa mwislamu kumkubali Yesu; maana maisha yao yote wamefundisha kila kitu kinyume na Yesu. Ukweli kabisa si kwamba hawataki kwenda mbinguni bali, kama asemavyo Paulo, "wana juhudi sana" bali tu si katika usahihi.

      Inahitajika NEEMA TU ya Mungu kumtoa katika kifungo hicho. Tuwaombee.

      Ubarikiwe ndugu yangu.

      Delete
  4. Replies
    1. Hata waswahili husema "Ukweli unauma." Mtu yeyote anayelemewa na "KWELI" lakini hayuko tayari kuukubali huishia kujawa na ghadhabu, kuchukia, kutukana na mambo kama hayo, maana moyoni anajua kabisa kwamba hii ndiyo njia sahihi; lakini iko roho nyingine iliyomfunga na inamzuia kuifuata kweli.

      Walio ndani ya Kristo hawatishwi na matusi wala kitu chochote. Kwanza unazidi kutuongezea tu pointi. Wewe tukana upendavyo, wala hata hayaingii moyoni. Tunaendelea tu kumfurahia Mwokozi Yesu Kristo.

      [USHAURI WA BURE: JIBU HOJA KWA HOJA KAMA UNAZO - KUTUKANA HAKUKUSAIDII; SANASANA UNAZIDI TU KUMWAIBISHA MUNGU WAKO; MAANA UNAONYESHA KUWA HANA MAJIBU NDIYO MAANA UNAKUWA FRUSTRATED NA "KWELI"].

      Bwana Yesu akubariki.

      Delete
  5. Hakika ukweli utabaki kuwa ukweli sidhani kama mtu unaujuwa ukweli kuna haja gani ya kuingiwa na gadhabu? bali ni kuukubali na kubadilika ili siku itakapokuja usijilaumu, ndugu yangu mungu akuonye kweli upate kubadilika. AMEN

    ReplyDelete
    Replies
    1. Amen ndugu. Mtu akishindana na Kweli anapata wakati mgumu sana maishani mwake. Kumbe jibu ni kama usemavyo: "kuukubali ukweli." Hakika kabisa!

      Delete
  6. Inaumiza sana! Uislamu ndo dini ya haki!

    ReplyDelete
    Replies
    1. nakuelewa rafiki. lakini Mungu ni mwema; iko siku utafahamu ukweli wa mambo kwamba hakuna njia ya kwenda mbinguni KAMWE nje ya Yesu Kristo. HAKUNA! HAKUNA! HAKUNA!

      Kwangu pia inaumiza mno mno kuona mamilioni ya wanadamu wakiingia kuzimu kwa sababu ya kudanganywa. Najua hutaamini kwa sasa, lakini KAMA MUNGU AISHIVYO, hakika kabisa, HAKUNA HATA MWISLAMU MMOJA ATAINGIA MBINGINI KWA TIKETI YA UISLAMU! HAKUNA!

      Namwomba Mungu wa mbinguni akupe ufunuo rohoni mwako wa nini maana ya maneno haya; maana mimi kama mwandamu sina jinsi ya kukufanya uelewe.

      Mungu akubariki na kukusaidia katika Jina la Yesu.

      Delete
  7. eewe ndugu yangu aliye kimbia dini ya uislamu nakuhurumia na nakusitikia mno!!!! ww umekimbia tu ili maneno ya mnyezi mungu yatimie,kwamba mkafiri huingia motoniiiiii.ewe ndugu yangu tafakari na urudi katika dini hii ili ujiepushe na moto wa jahanamu!!!!!'!!

    ReplyDelete
    Replies
    1. Yesu anakuita na wewe uokoke kama Ibrahimu ili akupe uzima wa milele kuliko kujaribu kuununua uzima huo kwa juhudi za kibinadamu; jambo ambalo hakuna mwanadamu anayeliweza.

      Ibrahimu alishaona UZIMA si rahisi akarudi kwenye dini, maana dini haziokoi na wala hazina faida. Wewe hujawahi kuokoka, ila yeye anafahamu pande zote mbili --- UISLAMU na WOKOVU WA YESU--- kwa hiyo, yeye ndiye aliye kwenye nafasi nzuri zaidi ya kukushauri na sio wewe kumshauri.

      Unachokijua wewe, naye pia anakijua; lakini anachokijua yeye sasa, wewe hukijui, sasa inawezekana ukawa na ushauri juu ya kile anachokijua sasa?

      Yesu anakupenda na anakuita uje kwake.

      Delete
  8. Inawezekana kweli Uislamu ni dini ya haki, lakini je ni dini y
    a upendo?, maana MUNGU NI PENDO anaiwa PENDO sio HAKI.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Shalom Robert,

      Uislamu SIO dini ya haki kabisa kulingana na Biblia. Maandiko yanasema:

      (2 Kor 5:21) Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ILI SISI TUPATE KUWA HAKI YA MUNGU KATIKA YEYE.


      (Rum 1:16-17) Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. Kwa maana HAKI YA MUNGU inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani.


      Kwa hiyo, hiyo si dini ya haki ya Mungu. Wao huchanganya siasa na dini. Kwenye maandamano yao utakuta wanadai mambo ya kisiasa na wanayaita haki. Mungu hahusiani na mambo hayo. HAKI inapotajwa kiroho inamaanisha KUWA NA UHALALI WA KUINGIA MBINGUNI. Na uhalali huo unapatikana kwa Imani katika Yesu Kristo kwa njia ya Injili yake.

      Ubarikiwe na Bwana.

      Delete
    2. Ucpende kukurupuka kaka ang kwnz sura ya kwanza ktk qur.aan c rum n fat.ha so n bora ungeulza na c kukurupuka na umedanganya vby yaan acha uongooo

      Delete
  9. hivi nyinyi wakristo kwa akili zenu mnajua sisi Yesu hatumfahamu?sisiYesu tunamuamini na tunaamini kaja na Injiil,na Injiil tunaiyamini lakini sio hiyo iliyotiwa mikono na wanadamu.Hivi umewahi kusikia Qur-an kuna agano jipya na lakale?Qur-an imekamilika na ni kitabu kisicho nashaka ndani yake,hakika ni uongofu kwa wale wamchao Allah.Na hivi mkisema mtakwenda mbinguni mnaelewa ni kitu gani?au mnasema tu?na huyo Ibrahim wa misri katoa aya ya uwongo (Sura Yusuf 10) Inasema :Wito wao humo utakuwa: Subhanaka Llahumma "Umetakasika Ee Mwenyezi Mungu!" Na maamkio yao humo ni "Salama". Na mwisho wa wito wao ni: Alhamdulillahi Rabbil A'lamiin "Kuhimidiwa kote ni kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote"huyo Ibrahim wa Misri ni mzushi.Istoshe Qur-an haikusema kuwa waislam mtakwenda motoni..la hasha!Qur-an inasema katika surat-Bayyina aya ya 8 "Malipo yao kwa Mola wao Mlezi ni Bustani za daima, zipitazo mito kati yake. Wakae humo milele. Mwenyezi Mungu yu radhi nao, na wao waradhi naye. Hayo ni kwa anaye mwogopa Mola wake Mlezi"
    Mtume Muhammad ndie alokuja na muujiza wa Qur-an na yeye makaazi yake ni Peponi."Allah tunakuomba waonyeshe ukweli hawa Makafiri"Aaammin

    ReplyDelete
  10. Ninyi waislamu hamuiamini Injili . kama kweli mngekuwa mnaiamini injili mngekuwa mnabatizwa kama injili inavyoagiza

    ReplyDelete
  11. PRAISE THE LORD, EMMANUEL "GOD WITH US",i would like to congratulate you mr.ibrahim, for stepping towards the heaven kingdom, i think up to this time you have been proved about the kindness and politeness of our lord Jesus christ, he loves us, he cares us, always he bless us, he is the way and light to us and many things that lord Jesus gives us free, so am really interested with your prophecy

    ReplyDelete
  12. am really interested with your prophecy mr, ibrahim

    ReplyDelete
  13. Ww unaesema muhammad s.a.w yupomoton una ukakka au unaoongea tyu kwnza hakka dn mbele ya Allah n uislam xx mi cwaelew kbx na huyo ibrahim n muongo tn mungoo namkosoa vkal xn kwa aya alzosema ktk qur.aan asome tn na azrudie na azielewe kwanza qur.aan n ktabu cha kwel 2:1-4 billaah mi camn asemayo huyo ibrahm ila mi naona n sheitwan kamuonyesha huyoo na huyo hakuwa muislam bal alkuwa n mfano wa muislam na hakuisoma qur.aan ipasavyo na hakuwa na iman huyo 3:101,3:99,3:98,3:103,3:105,3:106.Ewe ibrahiim umepotea ndugu yng ulpo cpo kaka ang 3:112 daah innaa lillaah wainna ilayh raajiuun alokuroga kafa maana hata huyo issa bn maryam masih alsema baada yng mm atakuja mwngn nae ataitwa ahmad xx kwa nn waiendekeza nafc ya akhii ila najua cku pale utakapoingia ndan ya tumbo la ardh utasema lait nngejua ila ushachelewa maana mkrsto aksilimu anakuwa hana dhamb je ww uingie kwenye ukrsto c waitaka jahannam mwenyewe daah naona umeangamia km firaun n abii lahab

    ReplyDelete
  14. Na tunaiamn xn hio injil maana Allah kavteremsha vtabu vnne navyo n taurat mousa zabur daud injl issa na qur.aan muhammad na pia tunaiamn mitume yote cc hatubagui maana nguzo zetu za iman zpo cta na miongon mwa hzo n kuiamn mitume najua mshazoea kutuambia cc maneno mabaya ila Allah anasema mwenye kujiongezea maradh bc na yy Allah humuongezea maradh xx huyo ibrahiim ndo kaongezewa kbx kwnz mlshawah ona qur.aan inabadlka yaankuna qur.aan mpya n ya kale na mlshawah ona maneno ya Mola yanabadlka xx mbn nyny biblia imebadlka jaman mara agano la kale mara agano jpya so cwaelew na huko kubatza cc hatubatz kwa sababu kla chenye kuzaliwa ni islam ndo maana mnabatzwaa il mtoke ktk uislam na huyo ubrahiim alkuwa na shaka xn ktk uislam kwnz cc huwa hatulazmishan ktk dn uwe muislam ucwe muislam n juu yk 3:75 na hata huyo issa alwaambia watu wa izrail mwabudum Allah mola wng mm na mola wenu nyny so con haja ya mtu kukaa kutukash cc waislam mna dn yenu tuna dn yetu xx nn na huyo ibrahiim n mdhalim wa nafc kbx 3:94 na kama ameisoma vzr qur.aan aisome tn sura ya al imraan aielewe na mm nmeitumia hio sura coz nmeona ktk maelezo yk na hzo haya zake mbl alzozielezea ni uongo (tafsir)n bora angewaulza wana wazuon kuhusu hzo aya maana haraka haraka hutokana na sheitwaan 3:102 ,3:128 hlf uislam n dini ya aman na huyo dhki tyu zlmfanya awe mkrsto hana lolote ila narudia tn ww ulisema muhammad yupo moton una uhakka au unapenda lig cc tunamkubal yesu km mitume mingn

    ReplyDelete
  15. INNA LILLAH WAINA ILAYHI RAJIUN.... HUU NI MSIBA MKUBWA SANA UNAHAMA KWENYE MWANGA UNAKWENDA KWENYE GIZA... KABLA HUJAFA RUDI KATIKA UISLAM NDIO MFUMO SAHIHI WA MAISHA YA MWANADAMU HAPA ULIMWENGUNI

    ReplyDelete