Monday, May 13, 2013

Kutoka Kwenye Uislamu Hadi Kumkubali Yesu Kristo





Naeem alikuwa ni Mwislamu tangu utoto wake. Ulifika wakati ambapo alikutana na Yesu Kristo. Matokeo yake, aliweza kuyajua makusudi ya kuumbwa kwake. Na sasa anamshangilia Mwokozi na Muumba wake ampendaye, yaani Yesu Kristo. Je, ilikuwaje? Tafadhali soma ushuhuda wake ufuatao:

********************

Nilikua nikiwa Mwislamu. Nilikulia Mashariki ya Kati. Tulikuwa tukienda kuswali, hasa Ijumaa. Nakumbuka tulikuwa tukiswali swala tano kwa siku. Kila kitu tulichofanya kilihusiana na imani yetu.

Na ninakumbuka kukulia kwenye utamaduni huo, huku shauku yangu ikiwa ni kutaka kuwa na uhusiano na Mungu nikijua kuwa hii ndiyo dini na Allah ni Mungu na Muhammad ni mtume wake; na njia ya kufika kwa Allah ni kufuata mafundisho ya Uislamu, na maneno ya Muhammad, yaani Hadith.

Wakati nikikua, nilikuwa nawafahamu Wahindu, Masingasinga, hata Wakristo, Wakatoliki. Nina marafiki wa karibu ambao walikuwa Wahindu. Hivyo, huwa tunazungumza kuhusu dini. Lakini akilini mwangu, nilijua kuwa, kwa kuwa nilizaliwa na kukulia katika Uislamu, basi ningebakia tu Mwislamu.

Nilishasikia juu ya Yesu na injili; juu ya yale aliyotenda, lakini halikuwa ni jambo linalonivuta kwa sababu wakati ule, Uislamu kwangu haukuwa tu ni dini bali ni namna fulani ya utaifa. Hivyo, moyoni mwangu ingekuwa ni kama kichekesho kubadili utaifa wangu!

Pamoja na kwamba kulikuwa na mambo kadha wa kadha ambayo sikukubaliana nayo (kuhusu Uislamu), ukweli ni kwamba, Uislamu haukubali mtu kuwa na maswali na mashaka juu ya imani.

Kaka yangu alikuwa chuoni. Kwa hiyo alipokuwa akija wakati wa likizo, alianza kuongea kuhusu Ukristo. Alileta Biblia nyumbani. Tulianza kuwa na mijadala. Na wengi wa marafiki zake walikuwa wameokoka; wana uhusiano binafsi na Yesu. Walianza kuzungumza nami juu ya hayo. Nilikuwa napinga sana na sikutilia maanani.

Wakati hayo yakiendelea, nilikuwa nikienda na kaka yangu kwenye mikutano ya kila wiki. Niliona sinema kuhusu unyakuo wa kanisa ambayo ilinigusa sana. Na usiku ulipofika, walifunga kipindi kwa sala.

Nilikuwa nimekaa nyuma, labda kwa ujinga, au ujasiri au kiburi, nikasema, “Sijui kama wewe ni wa kweli. Siamini upuuzi huu. Lakini kama wewe ni wa kweli, njoo ujionyeshe kwangu.” Hiyo ndiyo iliyokuwa sala yangu.

Siku kadhaa baadaye nilikuwa niko chumbani kwangu kwenye saa tano hivi, nikiwa nimemaliza kusoma riwaya yangu, nikaweka kitabu chini, nikajinyoosha. Nikagundua kuwa chumba kilianza kuwa na giza. Si giza hasa lakini kilikuwa kinajaa namna fulani ya uovu. Nikawa nawaza, ni kitu gani kinaendelea hapa?

Wakati nikiwaza haya, kitu kilinishika begani na kunivutia kwenye mto kitandani. Kisha mwili wangu ulianza kuwa na mwitikio. Halafu mlango ukafunguliwa na mimi nikawaza labda ni kaka yangu.

Lakini badala yake kiliingia kiumbe ambacho baadaye nilikuja kujua kuwa alikuwa ni pepo. Alipokuwa akija kitandani kwangu, akawa anasema kuwa ataniua. Nikaamini kabisa kuwa akinifikia, ataniua.

Hapohapo nikawaza kuwa Allah ni Mungu wa Uislamu, je, anaweza kunisaidia? Kwa namna fualani, nikajua moyoni mwangu kuwa hili ni jambo ambalo haliwezi. Hivyo, nikawaza, je, Yesu anaweza kunisaidia?

Wakati nikiwaza haya, huyo pepo akawa anaendelea kuja kitandani kwangu. Alifika kitandani kwangu, kisha akatoweka; sikumuona tena.

Kile ambacho kilikuwa kimenishikilia pale kitandani nacho kikaniachia. Nikaweza kuamka tena. Nikainuka kitandani kwangu na kukimbia nje ya chumba na kwenda kumwamsha kaka yangu.

Nikamweleza kilichotokea. Akasema, “Je, ulikuwa ukiota?”
Nikasema, “Hapana. Yalikuwa ni maono halisi kabisa!” Nakumbuka nilimwambia, “Hata mabega yangu bado yanauma kutokana na kushikiliwa.”

Alianza kuzungumza na mimi juu ya jambo lile nami nikasema, “Ni sawa lakini ninaogopa. Nisaidie. Naamini hili jitu litaniua!”
Akasema, “Kuna mtu mmoja tu ambaye ana mamlaka juu ya mapepo.”
Nikasema, “Nani huyo?”
Akaniambia, “Ni Yesu.”
Nikasema, “Sawa.”

Usiku ule tuliomba pamoja na sala yangu ilikuwa, “Yesu mimi sikujui wewe ni nani. Sijui kama nikuite Bwana; lakini nahitaji msaada wako. Na nimeambiwa kuwa wewe tu ndio unaweza kuniokoa kwenye jambo hili. Kwa hiyo, nakupa maisha yangu.”

Kaka yangu aliniombea na nikajisikia vizuri lakini si vizuri kabisakabisa. Akasema, “Basi, tutaonana asubuhi.”
Nikasema, “Mimi siondoki, nalala humuhumu!”
Akasema, “Hapana. Nenda tu chumbani kwako. Inabidi umwamini Yesu na uende chumbani kwako.”

Kwa hiyo, nilienda chumbani kwangu, nikawasha taa zote, nikatoa Biblia ambayo kaka yangu alinipatia. Nikawa nasoma kitabu cha Yohana.

Ghafla, mwili wangu ukaanza kutetemeka. Nikasema, “Mungu wangu, amerudi tena!”

Nikajikuta hapo kitandani kwangu ninaangalia kwenye kona mojawapo ya chumba changu. Kukawa kuna nuru na nikawa nahisi uwepo ambao naamini ulikuwa ni uwepo wa Kristo. Na ninakumbuka nikiwa naangalia kwenye hiyo kona ya chumba, ilikuwa ni jambo la ajabu kwangu kwa sababu kulikuwa na amani kubwa sana kiasi kwamba ilijaza kabisa moyo wangu na kufunika kabisa mawazo na hisia zangu zote za hofu zilizokuwapo mwanzoni. Sidhani kama nimewahi kuwa na amani kama hiyo tena.

Nakumbuka nikawa naangalia tu. Kilichotokea, ile hali ikanilaza usingizi, na kama sikosei nilisema, ‘Safi sana (cool)’ – kitu cha namna hiyo.

Baada ya usiku ule, sikujua nifanye nini. Nilijua kuwa nimekutana na Kristo. Nakumbuka nilikuwa na mazungumzo na kaka yangu kuhusiana na wokovu; kuhusiana na kumwamini, kumkubali na kumkiri Yesu.

Nakumbuka hata wakati nilipokuwa nikiangalia TV, waliposema tuombe hiyo sala, nilikuwa nikiomba tena na tena. Nadhani niliiomba hata mara kumi!

Maisha yangu yalibadilika; hata mawazo yangu yamekuwa tofauti sasa. Mtazamo wangu kuhusiana na Mungu ulibadilika kabisa. Zamani, kwenye Uislamu, Mungu alikuwa mbali sana lakini sasa yuko karibu. Kwa Waislamu, hata ukimwuliza sasa, je, unakwenda mbinguni? Atakwambia kuwa hajui. Wanasema tu, inshallah, yaani Mungu akipenda. Lakini sasa ni tofauti. Ninajua kuwa ninao uhakika kwa imani.

Mwanzoni nilikuwa nikiwaza, labda ukifanya matendo fulani kwa kiwango fulani, basi unakuwa karibu zaidi na Mungu. Sasa hivi sihitaji kufanya hivyo. Matendo hayanifanyi kuwa karibu na Mungu. Ukaribu wangu na Mungu na upendo wangu na Mungu unaweza kukua. Lakini Yeye tayari yuko karibu kabisa nami.

Nadhani watu wanapenda mtu mwingine awafahamu kwa ukaribu kabisa. Ni jambo jema sana kujua kuwa Mungu anatufahamu kwa undani sana na anatupa makusudi ya maisha. Nadhani jambo kubwa kabisa kwangu ni kwamba, tangu nilipokutana na Kristo, nimeshajua makusudi ya mimi kuumbwa. Najua kuwa makusudi hayo ni kuwafanya watu wengi iwekenavyo wakutane na upendo alio nao.

Tafakari

Hoji mambo

Chukua hatua.

No comments:

Post a Comment