Friday, July 26, 2013

Yesu Aongea na Binti wa Kiislamu; Binti Aokoka





Sharoni hakuwa Mkristo bali alikuwa ni binti wa Kiislamu. Na wala hakuwa amewahi kujifunza habari za Yesu na Ukristo. Lakini Bwana Yesu mwenyewe alimfuata na kujidhihirisha kwake. Je, ilikuwaje, na nini kilitokea baada ya hapo? Tafadhali fuatilia ushuhuda huu wenye nguvu na unaodhihirisha upendo na uweza na uungu wa Bwana Yesu.

……………………………….

Jina langu ni Sharoni Sabina Natrajan. Kwa sehemu kubwa ya maisha yangu nilikulia Bombay. Familia yangu si Wakristo. Kwa hiyo sikuwahi kupata mafundisho yoyote ya Kikristo. Natokea kwenye familia ambayo inathamini sana elimu, na kila mtu ana elimu ya kutosha. Upande wa mama yangu, anatokea kwenye ukoo wa Zaminda. Na hata nyakati zile, wavulana na wasichana walikuwa na elimu kubwa.

Baba yangu ni injinia ambaye amesoma kwenye chuo kinachoheshimika sana, na anashikilia cheo kikubwa kwenye makampuni ya kimataifa hapo Bombay.

Sisi ni familia ndogo tu yenye mimi, dada yangu, baba na mama. Tangu nikiwa mdogo, nilikuwa ni mtu ninayependa masuala sanaa (creative arts). Nilisomea na kuhitimu katika sanaa za maonyesho na pia uchoraji. Kwa hiyo, maisha yangu yote ya utotoni yalikuwa yamejikita kwenye mambo haya.

Wazazi wangu walikuwa na upendo sana na nilipata kila nilichohitaji. Sikupungukiwa na chochote maishani mwangu.

Baba yangu alipenda sana nisomee uinjinia, licha ya kuwa wakati nikiwa sekondari ya juu nilikuwa tayari nikifanya sanaa za maonyesho kote nchini – kucheza ngoma, maigizo,n.k. Sasa, kwa kuwa alitaka niwe injinia, nilituma maombi na kupata nafasi kwenye chuo kizuri sana. Uinjinia haukuwahi kuwa jambo la moyoni mwangu, lakini nilifanya hivyo ili tu kuwafurahisha wazazi wangu. Kwa hiyo, nilienda Puna kusomea uinjinia lakini wakati huohuo nilikuwa nikifanya sanaa za maonyesho.

Nilipokuwa kule Puna katika muhula wa pili, kuna jambo lililotokea ambalo lilibadili kabisa maisha yangu. Nakumbuka siku moja nilikuwa chumbani peke yangu nikijisomea, maana mitihani ilikuwa karibu. Nakumbuka vizuri sana siku hiyo nilikuwa ndani, naandika huku nimefunga mlango kwa ndani ili nisisumbuliwe na watu.

Ghafla, nilisikia sauti ikiniambia niombe! Cha kwanza nilichofanya ilikuwa ni kugeuka na kuangalia. Nilipogeuka na nikawa sioni mtu, cha pili kilichotokea ni kuingiwa na hofu ya kwamba labda nachanganyikiwa! Inakuwaje nasikia sauti? Kuna kitu kisicho kizuri hapa!

Niliamua kuipuuza ile sauti na kuendelea kusoma. Lakini sauti ile iliniita tena jina langu na kunitaka niombe! Sikuwa na uwezo wa kuipuuza tena sauti ile ambayo iliendelea kunijia, ungedhani iko kila mahali kunizunguka.

Niliangalia saa yangu nikakuta ilikuwa ni saa 7:30 mchana. Na nikakumbuka kwamba katika kukua kwangu, wazazi wangu walinifundisha dini yao. Nami nilikuwa nikifanya yanayotakiwa kwenye dini hiyo lakini kama mazoea tu kulingana na hayo niliyofundishwa.

Walinifundisha namna ya kuomba lakini katika muda maalum. Kwa hiyo, nilipoangalia ile saa yangu, niligundua kuwa muda wa swala ulishapita. Na sikujua namna ya kuomba. Nilikaa tu pale nikiwa nimechanganyikiwa huku sijui cha kufanya. Wakati huohuo sikuwa na uwezo wa kuipuuza ile sauti.

Kwa hiyo nilifunga tu macho yangu na kukaa tu pale; kisha nikasema moyoni mwangu kwamba, “Sijui huyu ni nani anayenitaka niombe, lakini kama kuna Mungu kwenye dunia hii, nataka nikuone. Sijawahi kukuona; sijui kama kuna Mungu au hakuna Mungu. Lakini kama kuna Mungu na ni halisi, basi nataka kumwona Mungu wa kweli.”

Nilisema tu hivyo moyoni mwangu na kwa mara ya kwanza maishani mwangu, macho yangu yakiwa yamefungwa, niliona maono. Nilimwona mtu amesimama mbele yangu. Kulikuwa na nuru kubwa. Sikuweza kuona uso wake. Lakini nilitambua mara moja moyoni mwangu kwamba huyu alikuwa ni Yesu! Hakukuwa na shaka yoyote. Yeye hakusema kuwa ni Yesu lakini nilijua tu kuwa huyu alikuwa ni Yesu.

Kilichofuata hapo nilijikuta nimepiga magoti na machozi mengi yakawa yananibubujika. Kulikuwa na upendo mkubwa uliokuwa unatoka kwake. Nilikuwa nashindwa kujizuia kulia; niliendelea tu kulia. Pia ilikuwa kama vile naweza kutazama moyo wangu; na nikawa naona madoa mengi meusi; mambo ambayo hata sikujua kuwa nilikuwa nayo. Nilitambua kuwa nilikuwa nina kiburi kikubwa; nilikuwa mwenye kujihesabia haki. Kila kitu kilikuwa sawa tu maishani mwangu na sikujua kabisa kuwa nilikuwa na hali hiyo ndani yangu! Nilikuwa mbinafsi sana. Nakumbuka nilipiga magoti na kulia na kusema, “Yesu, mimi sijui wewe ni nani lakini nakuhitaji katika maisha yangu.” Niliendelea kulia na kusema hivyo.

Baadaye alitoweka. Nilipofungua macho yangu na kuangalia saa, ilikuwa ni saa 8:15. Nikatambua kuwa kwa dakika 45 nilikuwa katika hali ile!

Baada ya hapo niliingiwa na woga. Niliwaza kuwa hapa ni lazima nimechanganyikiwa. Lazima kuna tatizo! Nilitoka mbio chumbani na jina lililonijia kwanza akilini mwangu lilikuwa la msichana mmoja ambaye alikuwa ni Mkristo pekee pale bwenini.

Nilienda kwenye chumba chake na kukuta amelala. Nilimwamsha na kumwabia, “Unajua, nilipoomba nimwone Mungu wa kweli, nimemwona Yesu! Kwa nini nimemwona Yesu wakati mimi si Mkristo?”

Nadhani na yeye aliogopa kunitazama maana macho yangu yalikuwa mekundu kutokana na kulia. Hakujua cha kufanya. Alikuwa ana Biblia. Alinipatia na kusema, “Soma kitabu hiki kama Yesu amejionyesha kwako.” Niliichukua ile Biblia na kurudi nayo chumbani kwangu. Na kuanzia saa 2 usiku nilianza kuisoma. Niliendelea kuisoma hadi saa 9 alfajiri! Sikuwahi kusoma kitabu kama kile maishani mwangu! Ilikuwa kama vile maneno yanaongea na mimi. Kilikuwa ni kitabu kilicho hai!

Kulipokucha, siku tatu zilizofuata zilikuwa ni kama vita kwenye mawazo yangu. Kwa nini nimemwona Yesu? Huyu Yesu ni nani?

Si kwamba kuna mtu alikuja kunieleza kuhusu Yesu. Sikuwa nimewahi hata kuingia kanisani! Nilichokuwa najua tu ni kwamba Yesu alikuwa ni Mungu wa Wakristo. Basi! Sikuwa na rafiki Mkristo; wala sikuwahi kuwa na shauku yoyote ya kumjua Yesu au kwenda kanisani kabla ya hapo. Na wala sikuwa namtafuta Mungu! Wala sikuwa napita kwenye jambo lolote gumu. Sasa kwa nini nimemwona Yesu?

Kwa siku hizo tatu, vita hii iliendelea kwenye akili yangu. Baba yangu alinifundisha mara zote kutumia akili yangu katika kutafuta mantiki ya mambo mbalimbali ili kutatua matatizo ninayokutana nayo maishani. Hicho ndicho nilichojifunza maishani mwangu. Lakini kwa jambo hili lililokuwa limenitokea, sikuwa na namna kabisa ya kupata mantiki yake; na wala sikuweza kujua cha kufanya kutokana na kile nilichokiona.

Kwa hiyo, baada ya siku tatu nilienda kwa huyu rafiki yangu tena na kumwambia, “Inabidi unieleze zaidi kuhusiana na huyu Yesu.” Hapo ndipo aliponipeleka kwenye mkutano wa wanafunzi.

Kuanzia siku hiyo, nilianza kusoma zaidi Biblia na kujua mengi zaidi kuhusiana na Yesu. Mungu alifanyika kuwa halisi kwangu. Ghafla tu alikuwa hai maishani mwangu na niliweza kuwa na uhusiano na huyu Mungu. Niliweza hata kuonga naye; na kumwomba – si kama jambo la mazoea tu (kama zamani), lakini nilikuwa sasa na uhusiano naye kibinafsi sana.

Nilitambua kuwa, kama kuna Muumba, basi Muumba huyu ni lazima atataka kuwa na uhusiano na viumbe wake. Na hicho ndicho kilichotokea kwangu. Ilikuwa ni kama sasa nimeunganishwa na Muumba wangu.

Kadiri nilivyoendelea kusoma Biblia na kumjua zaidi Yesu, nilianza kuona mambo kwa namna tofauti kabisa. Nilianza kuelewa nini maana ya huruma, kusamehe, rehema. Mambo haya yalikuwa mageni kwangu. Sikuwahi kujua juu ya mambo haya kabla. Na maisha yangu yalibadilika. Nilianza kuwaona watu kwa jicho la tofauti; na Yesu akawa rafiki yangu.

Siku zilivyozidi kusonga mbele, sikuweza kuelezea mabadiliko haya kwa wazazi wangu, na wao nao mwanzoni hawakuweza kuelewa. Iliwachukua muda mrefu kuja kuelewa.

Nilifika mahali ambapo ilinibidi kufanya uamuzi mgumu. Wazazi wangu hawakutaka mimi nimfuate Yesu. Ilinibidi kuchagua kati ya kumwacha Yesu au kuwaacha wazazi wangu. Ikanibidi kufanya uamuzi mchungu sana wa kuwaacha wazazi wangu; na nilijua kuwa lingekuwa ni jambo la kitambo kifupi tu hadi pale nitakapopata uwezo wa kueleza mabadiliko yaliyokuwa kwangu. Na ujue, mabadiliko haya hayakuwa jambo la nje tu; lilikuwa ni jambo lililotokea ndani. Ilikuwa ni kama nimefunguka kwa namna fulani. Nilikuwa gizani na ghafla nikawa nimeona nuru.

Kwa hiyo, ulikuwa ni wakati mgumu sana nilioupitia ambapo sikuwa na mawasiliano yoyote na wazazi wangu. Lakini Yesu alikuwa pamoja nami wakati wote; na alinipeleka hatua kwa hatua maishani mwangu.

Nilikuja Chenai kutokea Bombay na nikaanza kufanya kazi kwenye sekta ya matangazo ya biashara. Nilikuwa nafanya vizuri sana. Nikaanza kushughulikia akaunti kubwakubwa za makampuni ya kimataifa. Lakini mara katika mwaka mmoja, kulikuwa na anguko la kiuchumi katika sekta hii. Makampuni yalikuwa yanafungwa. Ilinibidi nami niondoke kwenye kampuni yangu ili niende kufanya kazi kwenye kampuni nyingine.

Wakati ule nilikuwa nashughulika akaunti za mteja wangu mmoja. Hivyo, nilimwendea na kumwambia kuwa naondoka kwenye kampuni hii maana nimepata kazi kwingine. Mteja wangu alikuwa ni mteja mkubwa kabisa miongoni mwa mashirika ya umma nchini. Aliniangalia na kusema, “Ninafurahishwa sana na kazi yako. Ningependa uendelee kufanya kazi na sisi.”

Nilimtazama tu kwa mshangao na kujiuliza, “Nitaendeleaje naye ilhali kampuni niliyokuwa nafanyia kazi zake imefungwa?”

Akasema, “Kinachotakiwa ni wewe kuwa tu na kampuni kisha mimi nitakupatia kazi hizi zote.” Nilishangaa kweli! Hapo ndipo nilipoanzisha kampuni yangu mwenyewe ya matangazo ya biashara. Nakumbuka nilianzia kwenye duka la juisi. Nilikuwa nikikaa kwenye duka hilo na  kufanya kazi zangu. Nilimwambia mwenye duka, “Uwe unanipatia juisi kila baada ya saa mbili au tatu.”

Baada ya hapo hakukuwa tena na kugeuka nyuma. Kazi niliyoifanya kwa ajili ya ile sekta ya umma ilijulikana nchini kote! Kisha kazi zilifuatana moja baada ya nyingine. Niliweza kupata ofisi yangu mwenyewe. Ilifika wakati ambapo nilikuwa na watu 150 wanaofanya kazi! Baada ya hapo nilianzisha kampuni nyingine na Wamarekani wawili wanaoishi Wisconsin.

Katika yote haya, nimeona jinsi Mungu wangu; Yesu wangu alivyonisaidia. Maana nilipolazimika kuiacha familia yangu ili niweze kumfuata Yesu, wakati huo nilikuwa sina kitu. nilikuwa tu na elimu yangu basi. Kisha nilianzisha kampuni yangu ambayo ilikua kutoka hatua moja hadi nyingine.

Kwangu, ilikuwa ni Yesu pekee aliyeniwezesha kuyafanya yote haya. Aliniongoza kwenye safari yote maana Biblia ilifanyika kuwa kitabu changu cha kila siku. Niliisoma na kupata kila maelekezo, na kutiwa moyo, na kutiwa hamasa. Ilinipa matumaini; ilinipa uzima mpya. Kila kitu kuhusiana na maisha nilikikuta kwenye Biblia. Na hivyo ndivyo nilivyotoka ngazi moja hadi nyingine.

Hatimaye, mimi pamoja na baadhi ya marafiki zangu na mume wangu ambao nilikutana nao Chenai, tulithubutu kuanzisha chuo cha sanaa na ubunifu (art and design).

Ninapotazama nyuma katika maisha yangu, naona kabisa jinsi ambavyo Yesu amehusika sana kuanzia wakati ambapo sikumjua Yesu na baada ya kumjua. Ilikuwa ni kama nimepata makusudi ya kuishi kwangu. Haikuwa kana kwamba nilikuwa natafuta kitu au kwamba mambo yalikuwa yanakwenda kombo maishani mwangu, hapana. Lakini kuanzia pale nilipomgundua Yesu, na kuanza kumjua, mambo yalibadilika. Maisha hayakuwa tena suala tu la kuwa na familia nzuri; elimu nzuri; kazi nzuri. Maisha yalikuwa sasa na makusudi; yalikuwa na maana. Nilikuwa nina maono kwa ajili ya maisha yangu. Hilo lilibadili mtazamo wangu mzima juu ya maisha.

Nilitambua kwamba Yesu si dini, bali ni halisi kwangu. Na cha muhimu kabisa, baada ya miaka 10, hatimaye nilipatana na familia yangu! Hivi sasa familia yangu wananikubali vivi hivi nilivyo. Wanaona mabadiliko yaliyo ndani yangu, na wananikubali hivi nilivyo. Haya yameweza kutokea kwa sababu tu ya imani yangu kwa Mungu wangu ambaye ni Yesu Kristo!

No comments:

Post a Comment