Friday, February 8, 2013

Kutoka Kwenye Uislamu Hadi Kwenye Ukristo



Jina langu ni Tahir na hii ni safari yangu kutoka kwenye Uislamu hadi kwenye Ukristo.

Mara baada ya kufika Marekani nikitokea Palestina miaka 14 iliyopita, nilimwoa msichana mzuri wa Kikristo. Msichana huyu alijaribu kuwa Mwislamu ili kunifurahisha mimi, lakini kadiri alivyojitahidi kufanya hivyo, ndivyo nilivyozidi kuwa mbali naye. Tulizaa mtoto mmoja, lakini ndoa yetu haikudumu maana ni vigumu sana kupenda wakati moyo wako umejaa chuki. Chuki ndicho kitu ambacho nilifundishwa wakati wa kukua kwangu kule Palestina – chuki dhidi ya Wayahudi, Wakristo na hata dunia nzima. Ukiwa kama Mpalestina, unafundishwa tangu ziku ya kwanza kwamba dunia yote ndiyo inayohusika na mateso yetu, na hasa Wayahudi na Wakristo.

Baada ya kuachana, baadaye mke wangu huyo wa zamani alikuja kuniambia kuwa amembatiza mwanangu. Nilikasirika mno kiasi kwamba nilienda kuingia moja kwa moja kanisani, nikamtukana mchungaji aliyefanya ubatizo ule, na nikamwambia kuwa angeenda jehanamu kwa sababu ya kitendo kile. Sikutaka kabisa mwanangu akue akiwa Mkristo!. Matokeo yake nilipigwa marufuku na mahakama kumtembelea mwanangu maana mke wangu alihofia kuwa ningeweza kuja kumteka mwanangu na kumpeleka Palestina. Hivi sasa sipati nafasi ya kumuona mara kwa mara.

Uzoefu wangu wa pili kuhusiana makanisa ulikuwa ni chuoni wakati mimi na rafiki yangu wa kike wa Kiarabu tulianza kujadiliana juu ya uwezekano wa kuwa Wakristo kwa kuwa tu tuliona ni dini isiyo na masharti magumu. Tulijua kuwa kile tulichokuwa tunakifanya ni kibaya na adhabu ya kuuacha Uislamu ni kupigwa mawe, lakini tulikuwa tunahitaji itikadi itakayohalalisha maisha yetu ya dhambi. Kutokana na ukaribisho tuliopata kutoka kwa msichana mmoja Mkristo wa Kiarabu kutoka pale chuoni, tulienda kutembelea kanisa lake Jumapili moja. Ibada ilikuwa imejaa furaha, jambo ambalo sikuwahi kuliona kwenye Uislamu. Baada ya ibada, tulipatiwa Biblia na kitabu kinachohusu Uungu wa Yesu Kristo. Miezi michache baadaye wakati wa mkesha wa Krismasi, tulitafuta kanisa ambako baadhi ya marafiki zetu wa Kiarabu walio Wakristo kutoka chuoni kwetu walituambia habari zake. Lakini tulishangaa kukuta limefungwa.

Nilikuwa na rafiki yangu aitwaye Khalil, ambaye tulikuwa tunazungumza pamoja juu ya maisha na hali ya dunia. Wakati mwingine tulikuwa tukijiuliza maswali kuhusu Uislamu na kushangaa kwa nini mambo ni hovyo sana kwenye nchi za Kiislamu. Tulikuwa tukijiuliza iwapo dini hii, ambayo hata hatukuifuata kikamilifu, ilikuwa ni dini ya kweli. Lakini maswali yetu hayakutufanya tufanye uamuzi wa mara moja. 

Nilioa tena. Safari hii ilikuwa ni ndoa ya kupangwa. Nilioana na msichana mmoja kutoka Palestina. Hii ilitokea baada ya familia yangu kunikatalia katakata kumuoa msichana wangu wa chuoni wakidai kuwa hakuwa safi kiasi cha kutosha kwa ajili yao. Nilimleta mke wangu mpya hadi Marekani, lakini nilikuta ni vigumu sana kumpenda maana hata sikuwa namfahamu vizuri. Kwa hiyo, nilikuwa nafurahi kwa sababu kazi yangu ilikuwa inanifanya niende mji hadi mji. Hiyo iliniwezesha kufanya mambo yangu ambayo hata hakuna haja ya kuyasema (ikiwa ni pamoja na kuwa na msichana kwenye kila mji.

Kisha Septemba 11, 2001, ilitokea.  Majengo pacha ya ghorofa yalipoanguka [kule Marekani baada ya kulipuliwa na ndege zilizobamizwa humo], heshima kidogo iliyokuwa imesallia kwangu juu ya Uislamu nayo iliporomoka yote. Suala hili lilinisukuma kabisa kwenye kuanza kuitafuta Kweli.

Niliachishwa kazi kutokana na hali ngumu ya uchumi iliyosababishwa na tukio la 9 -11. Wakati nikiwa kwenye mtandao wa intaneti kila siku kutafuta kazi, “kwa namna fulani”, kila mara nilijikuta nikiangukia kwenye mitandao ya majadiliano ya Kikristo. Na hata siku moja niliweza kupata Biblia ya Kiarabu kwenye mtandao.

Usiku mmoja wakati wa majira ya baridi nilijikuta nikisoma Injili ya Yohana. Sikuwa nikiiamini Biblia hata kidogo, maana nilikuwa nimefundishwa maisha yangu yote kuwa Biblia ni kitabu ambacho kimebadilishwa na wanadamu.

Lakini nilipoanza kusoma, nilishangaa. Nilianza kusoma juu ya Yesu na maisha yake mazuri, safi, yasiyo na dhambi, matakatifu, ya kushangaza, na ya kimiujiza, na sikuweza kuiweka Biblia ile chini. Nakumbuka nilisoma Injili ile yote mwanzo hadi mwisho. Nilipomaliza kusoma, ilikuwa tayari ni alfajiri! Nilikuwa nalia sana kiasi kwamba niliogopa kwamba ningemuamsha mke wangu. Sikutaka anione nikilia ili asije akaniuliza ni kwa nini ninalia.

Siku chache baadaye, nilifungua kompyuta yangu, na kwa sababu nisiyoijua, nikawa natafuta makanisa ya Kiarabu yaliyo kwenye eneo lile. Hatimaye nilipiga simu kwenye kanisa mojawapo. Upande wa pili, simu ilipokelewa na aliyepokea akaniambia kuwa baba yake alikuwa ndiye mchungaji, lakini alishakufa. Alinipatia namba nyingine ya kupiga – kwa mtu aliyeitwa Farooq. Huyu bwana ndiye mchungaji wangu hadi sasa na ni mtu ambaye Bwana amemchagua awe wa kunifikisha kwake. Tulijadiliana mambo mengi ya ndani kama vile tabia na haiba ya Muhammad, maisha yake, wake zake wengi aliooa na vita alivyopigana. Farooq alinipatia kitabu alichoandika ambacho kinalinganisha Uislamu na Ukristo, kikiwa na rejea kutoka kwenye Quran na Biblia.

Nilipoanza kusoma kitabu cha Farooq, nilipatwa na mshtuko pamoja na mshangao. Nilizitafuta rejea zote za Biblia na za Quran – zote zilikuwa sahihi – na sikuamini macho yangu! Nilitambua kuwa kumbe nilikuwa nimedanganyika maisha yangu yote! Jambo kubwa lililonivuta lilikuwa ni tofauti ya jinsi dini hizi mbili zinavyowatendea wanawake.  

Sikumbuki siku hasa ambayo Farooq aliniongoza kuomba sala ya kumpokea Bwana na Mwokozi, lakini ilikuwa ni kwenye mapema mwaka 2002. Ninaikumbuka fika siku niliyobatizwa. Ilikuwa ni siku ya ajabu sana na pia iliniogopesha! Na hivi sasa nimeshakuwa mtu tofauti sana tangu nilipomkubali Kristo.  Niko huru! Nimeshatambua kuwa hakuna kamwe ulinganifu kati ya Ukristo na Uislamu. Pale ambapo mwanzoni nilikuwa nina sheria na taratibu nyingi za kufuata kutoka kwenye Quran na Hadithi, hivi sasa nina uhusiano na Mungu. Ni tofauti kabisa. Uislamu unategemea kulazimisha, lakini Ukristo unaleta amani na upendo mwingi sana. Hivi sasa mimi ni mtu tofauti kabisa. Nimejitoa kikamilifu kwa mke wangu na ninaendelea kujifunza kumpenda. Hivi sasa, badala ya kwenda kwenye starehe, ninasoma Biblia. Ninahudhuria kanisani na kwenye masomo ya Biblia kila ninapoweza. Na sina chuki tena dhidi ya Wayahudi.

Nimekuwa nikimweleza karibu kila mtu ninayekutana naye huu ushuhuda wangu na imani yangu. Nilishawaeleza familia yangu, wafanyakazi wenzangu, na hata watu tu wa mtaani. Familia yangu hawakufurahia sana, hususani mke wangu ambaye bado hataki kukubali kwamba nimeshabadili dini. Anadhani kuwa iko siku fahamu zangu zitanirudia hivyo nitarudi kwenye Uislamu. Familia yangu, kwa upande mwingine, walijaribu kunirudisha kwenye Uislamu kwa njia ya hoja na mijadala juu ya Uislamu na Ukristo, baadaye wakaamua kunipuuza. Lakini hatimaye wakafika mahali pa kukubaliana na hali yangu kutokana na uhusiano mzuri na wa upendo tulio nao. Kama tungekuwa bado tunaishi Palestina, nina uhakika kuwa wangeshanikataa au hata kutishia maisha yangu.

Kwanza ujue kuwa, hata rafiki yangu, Khalil, naye ameshaukana Uislamu kabisa na anakataa kutii sheria na amri zake. Ninaendelea kufanya maombi kwa ajili yake ili aweze kuja kwa Bwana na kuwa huru mbali na yule mwovu.

Nilimpatia mke wangu nakala ya kitabu cha Farooq, lakini alipokisoma, alikwazika. Tafadhali, naomba  muombeeni ili aweze kuijua Kweli. Napenda tuende kanisani kama familia, lakini kama asipompokea Yesu, hii itakuwa ni ndoto tu. Hivi sasa ninahudhuria kanisani Jumapili asubuhi kila nafasi inaponiruhusu. Mke wangu kutokana na kujua kule ninakokwenda, huwa anapanga mipango muda wa mwisho mwisho ili mimi nishindwe kwenda.  

Ninapata “chakula” changu cha kiroho zaidi kupitia kusoma Biblia peke yake na kuwasikiliza wachungaji redioni ninapokuwa kwenye gari au kupitia intaneti.

Nilitaka kukujulisha kile ambacho Bwana amenitendea maishani mwangu. Kama umeshawahi kuwa Marekani kwa muda wa kutosha, utaelewa kuwa Wakristo si ‘Shetani mkubwa’ kama ambavyo umefundishwa.

Mimi ni uthibitisho kwamba maisha yanaweza kubadilishwa pale Kristo anapoangaza nuru yake gizani. Natumaini kuwa utatiwa changamoto ili uweze kuona na kujifunza zaidi kuhusu Kweli, kokote kule inakopatikana – iwe ni kwenye redio, TV, vitabu, au mtandaoni. Bwana Yesu na akuongoze katika kutafuta kwako Kweli.

Nakukaribisha  kuwasiliana nami.

Tahir

*****************
[Angalizo la blogger: Kama unapenda kuwasiliana na Tahir, fanya hivyo kwa lugha ya Kiingereza, si Kiswahili. Maana ushuhuda huu ni tafsiri kutoka Kiingereza. Unaweza kusoma ushuhuda huu kwa Kiingereza kwa kubofya HAPA.]

Tafakari!

Chunguza!

Jihoji!

Chukua hatua!

6 comments:

  1. Story za kutungwa,hazina kichwa wala miguu,achane kutunga story,mnaudhalilisha ukristo,inaonekana dini ya kupiga story za uongo,ili kupata wafuwasi.Kama ukristo ni dini ya kweli,Yesu asingepigwa na kupigiliwa misumari msalabani.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Habari yako rafiki.

      Stori za kutungwa ni zipi sasa? Ni hizi ulizsoma kwenye blog au ni Biblia unayoongelea. Ni vema basi ukionyesha ushahidi wa hoja yako. Vinginevyo wewe ndio unaonekana unaongea mambo ya kutunga. Ni maoni tu ambayo hayatokani na ushahidi bali ni mtazamo wako tu rafiki yangu.

      Ni nani aliyesema kwamba ili Ukristo uwe wa kweli NI LAZIMA YESU AWE HAKUPIGWA WALA KUPIGILIWA MISUMARI?

      Ni wapi ambako umeona mimi nimekukaribisha au kumkaribisha mtu yeyote aje awe mfuasi wangu? Si unaona jinsi ambavyo hoja yako haitokani na ushahidi wa kweli bali hiyo ndiyo ya kutunga?

      Hata hivyo, nashukuru kwa maoni yako na Mungu akubariki.

      Delete
  2. Aksante Shigongo wapili kwa story nzuri

    ReplyDelete
    Replies
    1. Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.(1Kor 1:18)

      Delete
  3. nipeni aya inayosema mabo yafuatayo

    1. ukristo dini
    2. biblia kitabu cha mungu


    alafu yesu hakusema mumuabudu, wala hakusema mumuchonge katuni la msalaba kisha mupambe makanisa.....wala mariam sio mama wa mungu....wala hamjaruhusiwa kubandika picha za yesu majumbani mwenu,yule sio yesu ni mzungu aliecheza filamu.....na biblia hakupewa nabii yoyote....na ukristo sio dini. mmekufuru ndugu zangu jipangeni na adhabu iliyo kubwa wallahi hamsalimiki

    ReplyDelete
    Replies
    1. Kama huna ufahamu juu ya dini au imani nyingine no heri kunyamaza kimya. Naona waislamu wengi wakifunguliwa mateso yao kupitia jina LA Yesu. Wanafurahia maisha mapya. Muislamu anajua hasa uislamu hawezi kunyoosha kidole kwa mkristo.

      Delete