Friday, May 3, 2013

Mwanamke wa Kiislamu Kutoka Palestina Aliyetokewa na Bwana Yesu na Sasa Ameokoka





Khalida ni mwanamke aliyekuwa Mwislamu, lakini baada ya kukutana na Bwana Yesu na kutembelea mbinguni, kila kitu kilibadilika kwake. Je, ni kitu gani kilitokea maishani mwake hadi kufikia kupelekwa mbinguni na Bwana Yesu? Tafadhali soma au sikiliza ushuhuda huu wa kweli wenye nguvu ambao utakuonyesha upendo, uweza, mamlaka na nguvu za Bwana Yesu, ambavyo vyote viko kwa ajili yako pia. Khalida anafanyiwa mahojiano na Sid Roth.

Sid Roth:
Khalida ni Mwarabu kutoka Palestina. Na sijawahi kusikia … sijui uliwezaje kupona, Khalida! Na una tabasamu usoni mwako … Ngoja niwaeleze kidogo kuhusu Khalida. Alipokuwa na umri wa siku 11, mama yake alikufa na baba yake alimtelekeza. Kisha alipelekwa kwenye nyumba ya mayatima. Alikaa humo hadi alipofikia umri wa miaka 9. Siku moja alitoka kwenda kutafuta maji ya kunywa, na bomu lililipuka kwenye hiyo nyumba na ile familia yake mpya iliteketea yote! Baada ya hapo watu hawakujua wampeleke wapi. Matokeo yake aliuzwa kama mtumwa. Huko utumwani alikuwa akipigwa na chakula alichopewa ni makombo tu.

Hatimaye askari walimwokoa na kumpeleka kwenye nyumba nyingine ya mayatima. Baadaye walimpata baba yake mzazi lakini alimkataa tena. Ni kukataliwa, kukataliwa, kukataliwa!

Kisha baba yake alimfanya mtumwa na Khalida alipofikisha miaka 15, alimwoza kwa nguvu. Baada ya kukaa na huyo mumewe na kuzaa mtoto, alipewa talaka na kufukuzwa. Kwa kuwa baba yake alikuwa bado hamtaki, alimwoza kwa nguvu kwa mume mwingine tena!

Khalida na mumewe mpya walienda Marekani. Lakini mume huyu alikuwa akimpiga hadi akamvunja taya! Kwa nini alifanya hivyo?

Khalida:
Alikuwa ni mtu mwenye hasira sana. Na katika Uislamu wanaume huwa wanafundishwa kuwa wanatakiwa kuwarekebisha wake zao. Kwa hiyo, alikuwa ananifundisha njia njema na alifanya hivyo hadi akanivunja taya. Hata hivyo sikujifunza chochote (kicheko).

Sid Roth:
Kwa hiyo, una watoto watatu na umeolewa kwa mume katili tena. Sielewi kabisa! Uliwezaje kuvumilia hayo yote? Si tu kwa mume huyo, lakini maisha yako yote! Uliwezaje?

Khalida:
Nilikuwa nikichukia sana. Kabla sijamjua Bwana nilikuwa nikighadhibika sana. Lakini ni kwa neema ya Bwana.

Sid Roth:
Halafu mambo yakawa mabaya zaidi. Alimwambia kuwa atamuua. Ulifanya nini kuhusiana na hilo?

Khalida:
Ilinibidi kukimbia kuponya maisha yangu.

Sid Roth:
Ulisikia sauti.

Khalida:
Nilisikia sauti. Kabla ya kusikia sauti ile, nilijaribu kujiua. Kisha nilisikia sauti ikisema kwa Kiarabu, “Ondoka gizani na uende kwenye nuru. Japo nilikuwa na hali mbaya niliamua kutii sauti ile maana niliona sina cha kupoteza.

Sid Roth:
Lakini angefanya nini mwanamke ambaye hazungumzi Kiingereza, hana fedha na ana watoto wadogo watatu akizunguka nao mitaani? Nini kilitokea?

Khalida:
Nilikutana na mama mmoja wa Kikristo ambaye alinichukua kama binti yake na akanieleza juu ya upendo wa Yesu.

Sid Roth:
Lakini wewe ulikuwa unaupenda Uislamu! Uliupenda sana Uislamu.

Khalida: Niliupenda …

Sid Roth:
Ulimpenda huyu mama kwa kile alichokutendea lakini hukumtaka Yesu wake.

Khalida:
Kweli kabisa. Tatizo langu siku zote lilikuwa kwamba, nawezaje kuamini kwamba Mungu ana mtoto; maana walitufundisha kwenye Uislamu kwamba Mungu hawezi kuwa dhaifu na kuwa na mtoto – hiyo ni ishara ya udhaifu. Kwa hiyo nilikuwa ninashindana na hilo. Nilitamani kuwa na upendo ule aliokuwa nao mwanamke yule; na huo ndio ukawa mwanzo wa kubadilika kwangu. Niliona furaha yake, niliona upendo wake, niliona maisha yake; na alikuwa kila wakati ameunganika na Mungu. Na nilikuwa nina kiu ya kuwa kama yeye.

Sid Roth:
Kisha uliamua kuwa huu ndio wakati ambao ninataka kuijua kweli. Hebu nieleze kile kilichotokea.

Khalida:
Nakumbuka nilikuwa nimeshachoshwa na kuwa katika hali ya kuchoka. Na ninakumbuka niliomba nikimwambia Yesu, “Kama wewe uko vile ambavyo watu wanasema kuwa wewe ni Mwana wa Mungu, basi nionyeshe. Uje kwangu na unionyeshe kuwa wewe ni Mwana wa Mungu!” Na sikutarajia kuwa kuna lolote lingetokea baada ya sala yangu ile. Lakini matokeo ya sala yangu ile rahisi yalikuwa ni kwamba, Yesu alinitokea na nikakutana na Bwana!

Sid Roth:
Hilo tu lingetosha. Lakini alienda hadi mbinguni. Je, uliona nini kule mbinguni?

Khalida:
Niliona kuabudu. Niliona jinsi ambavyo mbinguni wanamsujudia sana Yesu kama Mwana wa Mungu. Wanamwinua kama Mfalme. Baadhi ya mambo niliyoona – watoto, watu, viumbe, walikuwa wakitupa taji zao miguuni mwa Yesu. Alikuwa ana nguvu na mwenye utukufu.

Sid Roth:
Lakini haukujua kuwa mambo hayo yameandikwa kwenye Biblia?

Khalida:
Sikujua. Nilikuwa sijawahi hata kusoma Biblia kabla ya kukutana na mambo hayo. Nilichojua tu ni kwamba mambo yale yalikuwa halisi sababu yalikuwa wazi sana. Na nilikuwa sehemu ya mbingu; mambo yalikuwa halisi sana kiasi kwamba huwezi kuyapinga. Jambo moja mbinguni ni kuwa Yesu ni Neno la Mungu. Na kadiri unavyomtazama usoni, na uzima wake, na utukufu wake, ufunuo unakuwa wazi sana na halisi sana kiasi kwamba huwezi kuukwepa!

Sid Roth:
Na kinachonifurahisha ni kuwa (Khalida) sasa anaombea watu na wanapata miujiza – watu wenye kansa, wanapona! Lakini kinachonifurahisha hata zaidi ni baadhi ya ufunuo ambao aliupata kuhusiana na kuabudu. Na yeye humwabudu sana Mungu kuliko ulivyowahi kuona – kama unavyoenda kuona maana hata wewe unaenda kuwa mtu anayemwabudu Mungu.
Nikuombe Khalida umwabudu Mungu kama ambavyo huwa unafanya nyumbani kwako; ambako hakuna mtu mwingine ila Mungu tu.

Ninyi mlio hapa na ninyi mnaotazama, napenda mmwabudu Mungu. Kama mkifanya hivi, Mungu atajidhihirisha. (Khalida) hebu mwabudu Mungu.

Khalida:
Ndiyo. Napenda kuwatazama watu usoni na kuwaambia kuwa kuna nguvu pale unapozungumza kwa lugha ya mbinguni. Kwa kuwa tumeumbwa ili kumwabudu Mungu, tunapoingia kwa imani, ni lazima aonekane na Biblia inasema kuwa kutakuwa na uwepo wake.

Sid Roth:
Sasa hivi, kama unavyokuwa nyumbani, hebu mwabudu Mungu.

Khalida:
[anaanza kuomba kwa lugha ya mbinguni – Tazama 1 Wakorintho 14:2]. Ninapenda nitafsiri kile ambacho nilikuwa ninaomba. Nilichohisi kwenye roho yangu ni kumwinua Yesu juu ya kila kitu – juu ya hali yako, juu ya talaka yako, juu ya mashindano yako, juu ya ugonjwa wako, juu ya kila kitu unachopambana nacho kila siku. Unamwinua Mfalme wa wafalme juu ya hali yako na unakuwa kama Hajiri alivyokutana na Mungu na watu wengine kwenye Biblia. Kama sisi Waislamu tunapomwinua Yesu, tunakuwa waabudu wa kweli wa Mungu na tunakuwa wa kweli kwa Roho wa Mungu na hiyo ni silaha ya vita. Na kamwe hutashindwa katika mapambano yoyote kama ukimwabudu Mungu katika roho na kweli!

****************
Ndugu msomaji, umemsikia Khalida. Yesu Kristo ni halisi; na kila kitu ambacho Biblia inakisema kuhusiana na Yeye ni kweli, kweli, kweli tupu!

Tafakari.

Jiulize.

Hoji mambo.

Chukua hatua!

4 comments:

  1. ''Na wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule, msisadiki;''
    Haya, ni maneno ya yesu mwenyewe. Huyo mwanamke, kapagawa. Hajui alitendalo. Halafu, wakristo walioingia kwenye uislaam hawana hesabu.
    Hivi wewe ndugu yangu, kwa nini haushangai? Maana, karibu mataifa yote yanayoizunguka israel ni ya kiislam!

    ReplyDelete
    Replies
    1. Ibra rafiki yangu, waliopagawa hawako hivyo. Tazama hapa utaona mfano wa aliyepagawa: http://ajmacdonaldjr.wordpress.com/2012/05/28/demonic-activity-in-the-modern-world/
      Kuhusu watu kuingia kwenye uislamu, hilo sishangai hata kidogo. Watu wataendelea kuingia na kutoka kila mahali. Kuingia au kutoka si jambo la muhimu sana; cha muhimu umeingia wapi na mwisho wako ni nini? Yeyote anayetoka kwa Yesu na kwenda kuingia kwa mwingine anapotea HAKIKA. Mbingu ni za Yesu, sasa ukimkataa mwisho wa safari utaenda kwa nani?
      ………………………

      Na kuhusu kusadiki au kutowasadiki manabii, Bwana Yesu alisema hivi:

      BASI HAPO MTAKAPOLIONA CHUKIZO LA UHARIBIFU, lile lililonenwa na nabii Danieli, limesimama katika patakatifu (asomaye na afahamu),
      ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani;
      naye aliye juu ya dari asishuke kuvichukua vitu vilivyomo nyumbani mwake;
      wala aliye shambani asirudi nyuma kuichukua nguo yake.
      Ole wao wenye mimba na wanyonyeshao siku hizo!
      Ombeni, ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya sabato.
      Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.
      Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.
      Wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki.
      Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule.
      Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele.
      BASI WAKIWAAMBIA, YUKO JANGWANI, MSITOKE; YUMO NYUMBANI, MSISADIKI.
      Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. (Mat 24:15-27)
      ……………………

      Sasa nakuuliza hivi, Ibra, chukizo la uharibifu limeshaonekana? Wewe unaonyesha kana kwamba kila anayesema miujiza ya Yesu, kwa kuwa kwa akili za kibinadamu haieleweki, basi ni unabii wa uongo. Sivyo. Bwana Yesu yuko kazini usiku na mchana. Anatenda mambo makubwa sasa hivi ambayo kwa akili za kibinadamu huwezi kuyakubali. Mungu wa Biblia si Mungu anayeahidi na kusema, “Amini tu utajua siku ya mwisho.” Mungu wa Biblia anasema na kuishi na wanawe sasa hivi; anashughulika na mahitaji ya sasa pia – siyo ya baadaye peke yake.

      Delete
  2. Kaka James, Pole sana kwa kazi nzito ya kueneza injili na kuwavuta watu wengi kwa Yesu. Binafsi navutiwa sana na tafakari zako na huwa nikizisoma huwa napata nuru nzuri ya rohoni na naona kubarikiwa sana. Mungu azidi kukujaza kila aina ya neema na aendelee kufanya kazi ndani mwako ili yale aliyopanga kufanyika kupitia wewe yatimilike sawasawa na mapenzi yake. Ubarikiwe sana kaka.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Nakushukuru ndugu yangu kwa maneno yako ya kutia moyo sana. Mungu azidi kukubariki na kufungua moyo wako zaidi na zaidi. Asante kwa sala yako pia.

      Delete